Mcheza Taekwondo wa Tanzania aondoka na matumaini ya ubingwa katika mashindano ya dunia Korea Kusini

Muktasari:
- Omary mwenye uzito wa kilogramu 54 ataungana na wachezaji wengine 140 kutoka nchi 70 duniani kushiriki mashindano hayo ya Taekwondo.
- Omary amesema maandalizi aliyofanya yanatosha kujiamini na kuwa na uhakika wa kushinda.
Arusha. Mchezaji wa Taekwondo, Athuman Omary ameondoka nchini leo kuelekea Korea Kusini kushiriki mashindano ya dunia’ World Taekwondo Championship’ yanayotarajiwa kuanza Juni 23 hadi Juni 30.
Omary mwenye uzito wa kilogramu 54 ataungana na wachezaji wengine 140 kutoka nchi 70 duniani kushiriki mashindano hayo ya Taekwondo.
Omary amesema maandalizi aliyofanya yanatosha kujiamini na kuwa na uhakika wa kushinda.
“Tunawaomba wadau na serikali wajitokeze kutuunga mkono kwani mchezo huu una vijana wenye uwezo mkubwa, lakini bado hatujapata nguvu zaidi katika udhamini,”alisema
Makamu wa Rais wa shirikisho la Taekwondo Tanzania (TTF), Joseph Chuwa alisema maandalizi kuelekea michuano hiyo yamekamilika wanaamani mchezaji huyo ataiwakilisha nchi vyema.
“Ni mara ya kwanza kushiriki na tuna matarajio ya ushindi kwani kijana wetu amepata mazoezi ya kutosha na muda, tumefuatilia mbinu mbalimbali katika mishuano ya dunia na olimpiki iliyopita tumejiridhisha tutafanya vizuri pia kwa uzito alionao lazima tufanye vyema,”alisema Chuwa.
Ofisa michezo na Utamaduni jiji la Arusha, Benson Maneno alisema wanashirikiana na shirikisho la Taekwondo katika kuhakikisha mchezo huu unapiga hatua jijini hapa .
“Tunamshukuru katibu mkuu wa baraza la michezo Tanzania (BMT) kutoa kibali kinacho waruhusu kocha na mchezaji kwenda kushiriki mashindano ya dunia,” alisema Maneno.