Kinachoendelea mgomo wa wafanyabiashara Dar, Mwanza, Mbeya

Baadhi ya maduka yakiwa yamefungwa Kariakoo jijini Dar es Salaam. Picha na Aurea Simtowe

Muktasari:

Siku moja tangu mgomo wa wafanyabiashara wa Kariakoo uanze, mikoa ya Mwanza na Mbeya imeanza mgomo huo kwa madai ya utitiri wa kodi na tozo huku wakishinikiza mazingira amzuri ya biashara.

Dar/mikoani. Siku moja tangu mgomo wa wafanyabiashara wa Kariakoo uanze, mikoa ya Mwanza na Mbeya imeanza mgomo huo kwa madai ya utitiri wa kodi na tozo huku wakishinikiza mazingira mazuri ya biashara.

Dar es Salaam

Licha ya Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo kutangaza kusitishwa kwa ukaguzi wa risiti za kielektroniki (EFD), wafanyabiashara wameendelea kusimamia msimamo wao wa kutofungua maduka.

Hadi saa 3:30 asubuhi leo Jumanne Juni 25 2024 maduka mengi yalifungwa huku asilimia kubwa ya wafanyabiashara wakiwa hawapo nje ya maduka yao tofauti na ilivyokuwa jana.

Baadhi ya maduka yakiwa yamefungwa Kariakoo jijini Dar es Salaam. Picha na Aurea Simtowe

Maduka mengi yaliyofungwa ni yale ya nguo na bidhaa mbalimbali jambo linaloendelea kuleta vilio kwa wanunuzi kutoka mikoani na nje ya nchi.


Mbeya

Wafanyabiashara wa Soko la Kabwe na Mwanjelwa jijini Mbeya wamefunga maduka na kusitisha huduma leo Jumanne Juni 25, 2024 kwa madai ya utitiri wa kodi na tozo mbalimbali.

Mwananchi Digital imefika katika maeneo hayo na kushuhuhudia maduka yakiwa yamefungwa huku baadhi ya wananchi wakiwa wamejikusanya katika vikundi kusubiri hatima ya huduma.

Maduka ya Mwanjelwa jijini Mbeya yakiwa yamefungwa. Picha na Saddam Sadick

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Mkoa wa Mbeya (JWT), Charles Syonga amethibitisha kuwapo mgomo huo akieleza zipo sababu nyingi ikiwamo kodi na tozo mbalimbali.

"Sisi uongozi haujaelekeza chochote kwa mtu yeyote kufunga duka, tunajua changamoto zipo kama kodi na tozo mbalimbali, lakini kero zote zilishawasilishwa serikalini na tunasubiri leo agizo la mamlaka za Serikali.

"Kwa maana hiyo sisi tunawaomba warejeshe huduma wakati huu Serikali ikiendelea kulifanyia kazi suala hili kama ambavyo tumeona pale Kariakoo walivyofanya," amesema Syonga.

Maduka katika soko la Kabwe jijini Mbeya yakiwa yamefungwa baada ya mgomo wa wafanyabiashara. Picha na Saddam Sadick

Hivi karibuni kilio cha kodi na tozo mbalimbali kimekuwa kikisemwa zaidi na wafanyabiashara jijini Mbeya.

Awali, wamiliki wa maduka katika Soko la Mwanjelwa walifikia uamuzi wa kufunga biashara kabla ya Serikali kuingilia kati na kulimaliza.

Mwanza

Siku moja baada ya wafanyabiashara wa Kariakoo jijini Dar es Salaam kugoma na kufunga maduka, wafanyabiashara jijini Mwanza nao wamefunga maduka.

Baadhi ya maduka yakiwa yamefungwa jijini Mwanza. Picha na Mgongo Kaitira

Mwananchi Digital imepita katika maeneo mbalimbali ya jiji hilo na kubaini kutofunguliwa kwa maduka katika baadhi ya mitaa ikiwamo ya Kaluta, Rwagasore, Nyerere Plaza, Uhuru, Liberty na Kenyatta.


Endelea kufuatilia katika mitandao yetu ya kijamii

(Imeandikwa na Aurea Simtowe, Devotha Kihwelo, Mgongo Kitira na Saddam Sadick)