JWTZ kuwachuja waliokiuka usajili JKT, yatoa onyo walioghushi

Msemaji wa jeshi la wananchi nchini (JWTZ) Luteni Kanali ,Gaudence Ilonda katikati akizunguimza na waandishi wa habari jijini Dar es Saam kuhusiana na uandikishajji wa vijana wa Kujitolea wa JKT nchini. Picha na Said Khamis
Muktasari:
- Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) limesema litaendesha upya shughuli ya uhakiki wa vijana wanaoomba kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) ili kuwabaini wale walioingia kwa njia isiyostahili kuondolewa huku waliohusika kuwaingiza wakichukuliwa hatua za kinidhamu
Dar es salaam. Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) limebaini baadhi ya waombaji, viongozi wa Serikali na watumishi jeshini wanashiriki mbinu zinazokiuka utaratibu katika uandikishaji wa vijana watakaojiunga na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Kwa mujibu wa JWTZ, kuna kundi la wanaojiunga JKT kwa lazima na wale wanaojiunga kupitia kundi la kujitolea.
Tayari usajili unaendelea mikoa mbalimbali kupitia kundi la kujitolea baada ya JWTZ kutangazwa hivi karibuni.
Akizungumza na wanahabari leo Alhamisi Juni 27, 2019, Makao Makuu ya JWTZ Jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Habari wa Jeshi hilo, Luteni Kanali Gaudentius Ilonda amesema licha ya taratibu kuwa wazi, viongozi hao wanatumia nafasi zao kupenyeza ushawishi ili ndugu, jamaa au rafiki zao wasajiliwe.
Ilunda aliyezungumza kwa niaba ya Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Venance Mabeyo amesema kutokana na changamoto hiyo, JWTZ kwa kushirikiana na taasisi nyingine litaanza uhakiki wa vijana wote ambao tayari walishaandikishwa.
"Wakati kazi ikiendelea ya uandikishaji, tunaanza uhakiki upya kwa vijana wote walioandikishwa tayari, tukibaini umeghushi nyaraka, cheti cha kuzaliwa au vipimo vya afya tutachukua hatua za kinidhamu bila kuangalia sura, cheo au nafasi," amesema.
Kwa mujibu wa JWTZ, sifa za kujiunga na JKT ambazo nyingi zimekiukwa ni pamoja na kigezo cha umri unaozingatia makundi ya elimu ngazi ya darasa la saba hadi shahada ya uzamivu, afya njema, tabia njema, nyaraka na vyeti halisi vya elimu na uraia.
Kigezo kingine kilichoonekana changamoto ni idadi ya vijana watakaochukuliwa kujiunga JKT, kutegemea wingi wa vijana ndani ya mkoa husika, hivyo baadhi yao walikwenda kujiandikisha mikoa wasiyotambulika ngazi ya serikali za mitaa.