Dk Nchimbi kuhamia kaskazini kuzisaka kura za CCM
Leo Ijumaa, Septemba 12, 2025, mgombea mwenza wa urais wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Dk Emmanuel Nchimbi ataanza kampeni za kusaka ushindi wa chama hicho katika mikoa ya Kaskazini.
Dk Nchimbi ambaye amepumzika siku moja ya jana Alhamisi baada ya kufanya mikutano ya kampeni katika mikoa minane mfululizo anahamia Kaskazini ina
yojumuisha mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na Tanga kuendelea kusaka ushindi wa chama hicho.
Akiwa Arusha atafanya mikutano Longido, Arumeru Magharibi na atamalizia Arusha Mjini kwa kufanya mkutano mkubwa. Kesho ataendelea majimbo mengine ya mkoa huo kisha atasogea Kilimanjaro na baadaye Tanga.
Mikoa ambayo amekwisha kupita tangu alipoanza kampeni za kusaka kura za chama hicho Agosti 29, 2025 ni Mwanza, Mara, Simiyu, Shinyanga, Geita, Kagera, Rukwa na Katavi.
Katika mikoa hiyo, Dk Nchimbi aliwaomba wananchi ifikapo Jumatano ya Oktoba 29, 2025 kujitokeza kwa wingi kupiga kura kumchagua mgombea urais wa CCM, Samia Suluhu Hassan, wabunge na madiwani wa chama hicho.
Dk Nchimbi kwenye mikutano hiyo, amekuwa akieleza kile kilichofanyika miaka mitano iliyopita kwenye sekta za elimu, afya, maji, barabara na madaraja, uvuvi, kilimo na utawala bora.
Aidha, alieleza kile ambacho wanakwenda kukifanya miaka mitano ijayo huku akisema yeye amejiandaa kuwa msaidizi wa Rais Samia na watasukuma maendeleo kwa kasi zaidi.
Rais Samia yeye amekwishafanya mikutano katika mikoa ya Morogoro, Dodoma, Songwe, Njombe, Mbeya, Iringa, Singida na leo Ijumaa atakuwa Tabora na kesho Jumamosi, atahamia Kigoma.
Kampeni za uchaguzi mkuu, zilianza Agosti 28, 2025 na zitahitimishwa Oktoba 28, 2025.
Endelea kufuatilia Mwananchi.