Prime
FYATU MFYATUZI: Uchakachuaji, sorry, uchaguzi, acha mafyatu waamue

Kila fyatu anajua. Kuna mnyukano na mtanange usio ulazima baina ya mafyatu wanaotaka kutufyatua ili tuwape unene watufyatue na wengine wanaotuaminisha kuwa hawatatufyatua kama hawa wanaowafyatua wao ili watufyatue sisi baada ya kuwapa kura za kutufyatua.
Kwa sasa, Chakudema na Chakupindua wako pakanga wakifyatuana ili mwisho mmoja atufyatue na kuendelea kufyatua ulaji wa dezo. Ninachoona ni kamchezo kachafu sana kanakoweza kuchafua kaya ikafyatuka kiasi cha wanaotaka kuwafyatua wenzao nao wakajikuta wanafyatuliwa na wale wanaotaka kuwafyatua. Nani hajui kuwa tunaelekea kwenye ufyatuaji wa kura ya kula aka uchakachuaji? Ajabu, kati ya mafyatu hawa watafuta kutufyatua, mmoja amejipa mamlaka ya kumfyatua mwenzie! Hapa, napata kichefuchefu kuelewa. Je, hii kaya ni ya wanene au mafyatu? Jibu ni simpo. Hii kaya, kama tunavyofyatuliwa kuwa katiba inasema ni yetu, ni yetu. Sasa kama ni yetu, inakuwaje wao waamue kila kitu wakati sisi ndio tunapaswa kuamua kikatiba? Je, hii katiba wanaielewa au kulewa?
Kikatiba, pawa ni ya mafyatu wote, si ya wao peke yao, kama wanavyotaka kutufyatua wasijue wanaweza kutufyatua tukawafyatua kifyatufyatu.
Je, tunafyatuliwa changa la mato? Sasa, kama ni kweli siyo hivyo, inakuwaje wale wanaotegemea kuchaguliwa, washike kani? Nani kawapa hiyo pawa? Niulize. Kati ya ‘mteule wa God’, kama kweli, mwenye maono hata yasipoona kutokana na kupewa ujiko huu na wasioona.
Anapata wapi guts ya kumfyatua mwenzake lupango wakati wote ni waombaji wanaotegemea mafyatu tuwafyatue au kuwawezesha kufyatua ulaji?
Nani fyatu huyu ambaye amefyatua pawa zetu na kuzitumia vibaya kuwafyatua wapingaji wake nasi tukiangalia kana kwamba hiyo pawa siyo yetu?
Hakuna kitu kinanitisha kama kuona haki ya kuchagua na kuchaguliwa ni yetu mafyatu tunaofyatua kura za kula inafyatuliwa.
Nilidhani wao watatumia busara na kuacha kufyatuana ili wasitufyatue tuka fyatuka na kuwafyatulia mbali.
Nani kawapa pawa yetu? Je, wameikwiba, kuihodhi, kuifyatua, kuifuja, kuitukana, kuitukanisha, au kuipora? Kama ni hayo yote, mafyatu tunafanyaje?
Je, tukifyatuka tukafyatua kuna fyatu mfyatuliwa atatulaumu kwa kufyatuka na kumfyatulia mbali ili kulinda hadhi na haki yetu kama mafyatu waliogoma kufyatuliwa kienyeji? Chakudema wanazoza kuwa no reforms no election.
Chakupindua wanaronga no need for reforms but to deform the reforms of election reforms hata kama itachakachuliwa.
Who cares? Mambo yamefyatuka hadi mafyatu wanene wanaotaka tuwape unene tena watufyatue wanafyatuana lupango.
Hizi ni siasa au visasi? Ukipayuka ukweli, unatenda uhasi. Ukitenda uhasi, unazuia uhasi! Abishaye, akamuulize Tunda Lishe.
Despite all, Mafyatu wanataka siasa za kisasa ni siyo za visasi kama ilivyo kwa sasa ambapo ukale umegeuzwa usasa!
Tunataka siasa za siha siyo za silaha, ziwe za moto kama za ndata wanaonyaka wapingaji au usanii na usumbufu.
Kama kati ya washindani wawili, kuna mmoja anaweza kumsweka mwenzie lupango tena bila ya kosa lolote kifyatu.
Je, anaweza kumtendea haki kweli au kumfyatua kwa vyovyote viwavyo? Nimesikia hawa reformers wakitaka uchaguzi huru, haki, na uliokidhi kanuni na sheria. Tujalie wanaowaunga mkono wakawa wengi kuliko wanaounga mkono uchakachuaji wakaamua kukinukisha, bila kuchakachua, si watabwagwa tu.
Najua mafyatu siku hizi wanapenda kabumbu na kubet kuliko hata kazi.
Je, kama timu moja zinazopaswa kuchuana ikijitoa kutokana na kuogopa kuchezewa rafu, anayeamua kama timu iliyobaki ipewe ushindi au kupanga pambano upya ni timu kinzani au refa?
Je, katika hiki kipute na kitimutimu tunachoshuhudia, refa ni nani kati ya mafyatu na wenyewe wanaotaka kufyatua? Je, tumekubali kufyatuliwa kwa vile hatuwezi kufyatuka tukawafyatua waache huu ufyatu uchwara?
Je, kinachofyatua, ambacho siyo haki hata kama kikifanywa haki, tutegemee hawa wanaowafyatua wenzao bila aibu wanaweza kuwatendea mafyatu haki?
Je, hawa wanafyatuana ili kututendea haki au kutufyatua chini ya kisingizio cha kututendea haki isiyo haki?
Japo huwasikia wakiitaja na kuiongelea haki, sijui kama wanaijua.
Hata kama wanaijua, sijui kama waitenda.
Na kama wanaitenda, wanaitenda kwa nani zaidi ya wao wenyewe? Nani kawapa hiyo haki ya kufyatua au kuua kabisa haki za mafyatu wengine?
Je, haki ya mafyatu ni kuchagua mafyatu wa kuwafyatua au wa kupatikana kwa njia ya haki ili wawatumikie kwa haki au wawatumie wao na taasisi zao?
Je, haki ni ya mafyatu kuwafyatua wanaotaka kuwafyatua bila mafyatu kufyatuliwa kwa sababu ya kutaka kufyatua wanaotaka kuwafyatua kama moja ya haki zao.
Je, hapa wa kulaumiwa ni nani kati ya wale wanaotaka kuwafyatua mafyatu au mafyatu wanaogoma kufyatuka na kufyatua wanaotaka kuwafyatua?
Kwa kujua jinai inayoandalika tayari kuwafyatua mafyatu fyata siyo fyatuzi, mafyatu wataendelea kuufyata au kufyatuka na kufyatua lau kulinda heshima yao au kuiacha ifyatuliwe kama wao?