Prime
Fyatu kutoa gari kwa kila mpika kura ya kula

Kama mjuavyo, uchakachuaji, sorry, uchaguzi mkubwa umekaribia, na ninagombea urahis na lazima nitashinda hata kama ni kwa goli la mkono kama lile na Mapepe Tunaye. Hivyo, kwa vile mie ni muwazi, naweka wazi mikakati na ukarabati wa kushinda hii kitu mapema asubuhi kama ifuatavyo:
Mosi, kuanzia sasa, nitamwaga ndinga kali na za bei mbaya za kisasa kuhakikisha kila mpika kura anapata moja ili anipe kura ya kula. Mie, siyo wa kumwaga vikwata wala tukutuku visivyo na utukufu zaidi ya utukutu.
Si wa baiskili kama Sikiri maskini. Hivyo, kaeni mkao wa kula usawa huu wa kuvuna ambapo hamkupanda na kupanda ambapo hamtavuna.
Pili, nimeamua kukopa njulu nje na ndani kuhakikisha mradi wangu wa ushindi unafanikiwa.
Japo nimesikia baadhi ya mafyatu wakizoza na kupayuka kuwa nakopa sana, wanataka nifanye nini? Nani kawaamba kuwa kukopa ni kosa wakati ni harusi ingojeayo matanga ya kulipa kwa walipaji? Najali nini wakati sitalipa? Acheni kuuliza mambo haya nisiwapoteze bure.
Tatu, kuanzia sasa, nitatembelea kaya nzima kuanzisha na kukagua au kufungua ‘miradi’ ya kipwagu na pwaguzi ili kuwavutia wapika kura. Katika safari na ziara zangu, lazima nimwage njuluku kama sina akili nzuri.
Nne, nitakuwa mkarimu na mpole huku nikichanganyikana na mafyatu bila ulinzi kama ilivyokuwa kabla ya kuanza kampeni za kampani hadi waniamini na kuingia laini.
Nitaingia kwenye majumba yote ya ibada na kuwamwagia mamilioni. Natoa angalizo. Mnene wa dini yeyote, orijino au feki na ya kujipachika, atakayenipinga, nampiga stopu kwa kuchanganya dini na siasa.
Wajue, nitafunga maduku yao ya kuuza roho na neno. Atakayeniunga mkono na kunipigia ndogo ndogo, ruksa. Maana, huku si kuchanganya dini na siasa bali kudumisha amani na mshikamano japo kwa imani ya amani.
Tano, kila nitapozuru, lazima kutoa ahadi milioni kidogo bila kusahau kumwanga njuluku kwa wapika kura ya kula na kuwaahidi kwa kuwafyatua kuwa huo ni mwanzo tu ili wangie bila kujua kuwa, nikishaukwaa, nitawafyatua mkenge. Najua, mafyatu walivyofyatuka, watanipa.
Na wakinipa, sitawapa baada ya kupewa. Watajua kuwa hawajui na wakijua hawatajua kuwa hawakujua.
Sita, nitaanza ‘kukemea na kukoromea uoza’ ili kuwafanya mafyatu waote kuwa kaya yenye haki na tajiri kuliko zote duniani.
Mfano, kila niendapo, nitatoa takwimu za kupikwa kuwaweka sawa.
Nitawambia kuwa mimi ni muaminifu kuliko hata malaika na kwa Joji Kichaka na Trumpet, ndiyo maana nakopesheka.
Saba, kwa vile sina wapinzani wa maana, nitawakandia wapingaji, ambao wengi wao wako mfukoni mwangu, kuwa hawaaminiki kama mimi japo wote, kiukweli, hatuaminiki sorry, tunaaminika. Nitawasilibia na kuwakandia kinomi.
Nitasema kuwa wao wakipata ulaji, wataanza kuwatumia badala ya kuwatumikia. Watadanganya badala ya kuwaambia ukweli, kuwadhalilisha badala ya kuwaheshimu, kuwaibia badala ya kuwa waangalizi wa njuluku na mali zao.
Nitasiliba zaidi na kusema kuwa wao wanawaita funza badala ya mafyatu kiasi cha kuwaburuza badala ya kuwashawishi, kuwatesa badala ya kuwadekeza, kuwatenga badala ya kuwaunganisha.
Nane, nitaamuru magazeti yangu ya umbea kunipamba kuwa hajawahi kutokea kiongozi kama mimi tangu dunia kuumbwa. Hivyo, mafyatu wakinyima kura, wajue, wanajitia kitanzi wenyewe.
Pamoja na kuwa njuluku nitakayotumia ni ya mafyatu, nitawaambia wapambe na waimba mapambio yangu waseme kuwa hii ni njuluku ya Fyatu kila ninapotoa njuluku.
Tisa, nitahubiri amani na mshikamano katika kupeana ulaji lakini si katika kula. Hivyo, yeyote anayenipinga, anapinga amani, maendeleo, na mshikamano wa mafyatu.
Kumi, nitapiga marufuku mikutano ya wapingaji na wapinzani wangu iwe ni wa wazi au kwa kificho. Nitaamuru wakubwa wa ndata za mafyatu kuvuruga mikutano ya wapingaji iwe ni kwa kuwakataza, kuwachelewesha, au kuwapa maeneo yasiyovutia ili niwapige chini kirahisi japo nao si wapingaji bali wasanii wanaotafuta ubwabwa na kutaka kuuma umma wa mafyatu. Hamjawasikia wala mafyatu wa chata la Chakuuma?
Je wanawauma nani kama siyo mafyatu waliogeuzwa ubwabwa? Mtawaona wakidemadema na kusepasepa msijue kuwa kinachoitwa pilau si kingine bali nyinyi muhongwao udohoudoho na kuishi kwenye uchochole tokana na kughairi kufyatuka, kuendekeza tamaa, na uzwazwa hadi mkafyatuliwa kizwazwa.
Nani awezaye kumvua samaki bila chambo au kwa chambo kitupu? Thubutu yako? Nioanavyo na nijuavyo, japo samaki ni hayawani, ni wajanja kuliko mafyatu wanaofyatuliwa kizwazwazwa hivi.
Japo mafyatu nitakaowafyatua wanadhani wananifyatua, ukweli tutauona nikiisha ukwaa na kuanza kuwafyatua bila huruma. Nadhani hawa hawanijui uzuri.
Mwisho, nitachapisha mabango makuuuubwa tena ya mabilioni na kuyaweka kila mahali ili mafyatu wanione na kunipa. Najua. Wap viherehere wakataotaka kuhoji namna nilivyotengeza huu ukwasi na ninanunua nini. Hawa wasiwape taabu. Nitawazushia kesi kibao na kuwasweka lupango hadi mtiti uishe na kupita ndo niwaachie waendelee kupayuka huku mie nikikamua.
Du! Kumbe naota!