Wanandoa wauawa, miili yao yatupwa mtoni

Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Nicodemas Mwangela
Muktasari:
Ni wakazi wa Mlowo mkoani Songwe, Jeshi lawataka wakazi wa eneo hilo kuwa watulivu wakati uchunguzi ukiendelea
Mbozi. Watu watatu wakiwamo mume na mke wake, wakazi wa Mji mdogo wa Mlowo wilayani Mbozi Mkoa wa Songwe wamekutwa wameuawa na kisha miili yao kutupwa chini ya daraja la Mto Mlowo.
Waliofariki ni Luka Humri, Bahati Mohamed na mwingine ametambulika kwa jina maarufu la Mama Dina.
Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Nicodemas Mwangela amesema tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia leo Septemba 7, 2018 na mtu wa tatu ni jirani wa mume na mke waliouawa.
Alisema wauaji hao baada ya kutekeleza tukio hilo wamewachukua kisha kwenda kuwatupa kwenye daraja la mto huo.
Mwangela amewaomba wakazi wa Mlowo kuwa watulivu wakati jeshi la Polisi likiendelea na uchunguzi wa tukio hilo.
“Niwaombe sana ndugu zangu hebu kuweni watulivu kutokana na tukio hilo baya kabisa. Lakini wakati vyombo vya ulinzi na usalama vikiendelea na uchunguzi wa kiini juu ya watu hawa kuawa, niwaombe tena toeni ushirikiano kwa vyombo hivi kwa yoyote kutoa taarifa zinazohitaji ili kuwabaini waliotekeleza mauaji haya,” amesema.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe, Mathias Nyange amesema wanandoa hao walikuwa wafanyabiashara katika Soko la Sokowo na chanzo cha mauaji hayo bado hakijafahamika lakini upelelezi umeanza ikiwa ni pamoja kuwatambua kwa majina marehemu hao.
Mkazi wa Mlowo, Joseph Mwashiuya amesema tukio hilo limewashtua na kuufanya mji kutikisika kwani sio la kawaida na kuiomba Serikali kuimarisha ulinzi wakati huu.