Wafungwa wa Tanzania sasa kupiga kura

Muktasari:
- Mahakama Kuu imebatilisha kifungu cha Sheria ya Uchaguzi kinachowazuia wafungwa kupiga kura.
Dar es Salaam. Mahakama Kuu nchini imesema kuwa wafungwa wa makosa ya kawaida ya jinai wana haki ya kupiga kura katika uchaguzi mkuu.
Mahakama hiyo imetamka haki hiyo baada ya kubatilisha kifungu cha 11(1) (c) cha Sheria ya Taifa Uchaguzi kinachoweka zuio kwa wafungwa wanaotumikia adhabu ya kunyongwa na wanaotumikia adhabu ya kifungo cha kuanzia miezi sita.
Hukumu hiyo imetolewa na Jaji Elinaza Luvanda leo Desemba 22,2020 inatokana na shauri la Kikatiba lililofunguliwa na raia wawili, Tito Magoti na John Tulla ambao walikosa haki ya kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 kutokana na kuwa mahabusu.
Magoti na Tulla walifungua shauri hilo Mahakama Kuu Masjala Kuu, mwaka huu dhidi ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na Jeshi la Magereza.
Walikuwa wakidai kuwa kifungu hicho kinakinzana na Katiba Ibara ya 5(1) ambayo inaeleza kuwa Kila raia wa Tanzania mwenye umri wa miaka 18 anayo haki ya kushiriki katika Uchaguzi Mkuu.
Hata hivyo, ingawa kifungu hicho hakiweki zuio la utekelezaji haki hiyo kwa mahabusu wanaosubiri usikilizwaji wa kesi zao, lakini Jeshi la Magereza halijaweka utaratibu unaowawezeaha mahabusu kutekeleza haki hiyo.
Ingawa wadaiwa wakati wa usikilizwaji wakipinga madai hayo, walidai kuwa NEC imekuwa ikiwawezesha raia wote kutekeleza haki hiyo kwa mujibu wa sheria, lakini Jaji Luvanda katika uamuzi wake amekubaliana na hoja za Wakili Seka kwa niaba ya wadia kuwa kifungu hicho kuweka zuio hilo kwa wafungwa wote wanaotumikia adhabu kuanzia miezi sita kinakiuka Ibara ya 5(1) ya Katiba ya Nchi.
Amesema kuwa haki ya kupiga kura ya mahabusu wenye umri wa zaidi ya miaka 18 ihifadhiwa na kulindwa na Katiba.
Pia Jaji Luvanda amesema kuwa ingawa Ibara ya 5(2), imesema kuwa Bunge linaweza kutunga sheria kuweka sharti la kuzuia raia wa Tanzania kutekeleza haki hiyo, lakini Bunge kwa kuweka sharti ya zuio kuzingatia kifungo limekwenda nje ya muktadha wa Ibara hiyo ya Katiba.
Amefafanua kuwa Bunge lingeweza kuorodhesha makosa makubwa ya jina ambayo mtu akitiwa hatiani anaondolewa haki hiyo kama vile makosa ya uhaini na mauaji ambayo adhabu yake ni kunyongwa.
"Hivyo natamka kwamba kifungu cha 11(1) (c) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi Sura 343, Marejeo ya mwaka 2015 ni kinakinzana na Katiba na ni batili."