Vijana kufundishwa namna ya kuongeza thamani madini ya Tanzanite
Muktasari:
- Katika mpango wa Serikali kuendeleza ujuzi , itawapa mafunzo ya kusanifu madini ya Tanzanite vijana ili kuongeza ajira na kuyaongezea thamani kabla hayajasafirishwa katika masoko ya kimataifa.
Simanjiro. Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Vijana, Anthony Mavunde amesema watashirikiana na Wizara ya Madini kuwapatia mafunzo vijana ya kuongeza thamani madini ya Tanzanite.
Akizungumza wakati akifungua Tamasha la ubunifu kwa wanawake na vijana leo Ijumaa, Julai 05,2019 lililoandaliwa na Mbunge wa Viti Maalumu mkoa wa Manyara, Esther Mahawe, alisema mpango huo unalenga kuwapa ujuzi vijana Mirerani ambalo ni maarufu kwa biashara ya Tanzanite na mikoa mingine nchini.
Amewataka vijana na wanawake kujiunga kwenye vikundi ili kupata fursa ya mikopo kwenye halmashauri na ruzuku mbalimbali zinazotolewa kwaajili ya kuwawezesha kujikwamua kiuchumi.
Mbunge Mahawe amesema ameamua kuzunguka kwenye wilaya zote za Mkoa wa Manyara kuibua hamasa ya ujasiriamali na vipaji kwa vijana, kusudi watumie fursa za mikopo na masoko kujiendeleza kiuchumi.
“Mimi ni mfano halisi wa mhitimu katika Chuo cha Ualimu, lakini nilikosa ajira, sikukata tamaa bali nilitafuta mkopo wa Sh500,000 nikaanzisha shule ya watoto ambayo sasa hivi imekua kubwa na mwaka jana imetoa wahitimu wa kwanza kitado cha nne,” amesema Mahawe.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, Yefred Myenzi amesema katika Mwaka wa fedha 2018/2019, wametoa Sh230 milioni ikiwa ni mikopo kwa wanawake, vijana na walemavu ambayo ni mapato ya ndani.