Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Utalii wa Zanzibar waongeza watalii Hifadhi ya Mikumi

Watalii kutoka Zanzibar wakipanda magari, kutoka uwanja wa ndege Kikoboga uliopo ndani ya Hifadhi ya Mikumi tayari kuanza safari ya utalii ndani ya hifadhi hiyo. Picha na Bertha Ismail

Muktasari:

  • Hiyo imebainika baada ya watalii wengi wa kimataifa wanaotembelea Hifadhi ya Mikumi iliyoko mkoani Morogoro hutokea  Zanzibar na kutua moja kwa moja kwa usafiri wa ndege kwenye  hifadhi hiyo.

Morogoro. Kukua kwa sekta ya utalii Zanzibar, imekuwa neema kwa Hifadhi ya Taifa ya Mikumi baada ya kuongezeka kwa idadi kubwa ya watalii katika hifadhi hiyo iliyopo Kusini mwa Tanzania.

Hiyo imebainika baada ya watalii wengi wa kimataifa wanaotembelea Mikumi iliyoko mkoani Morogoro, kutokea visiwani humo.

Watalii hao ambao hufika kutembelea Visiwa vya Zanzibar, huunganisha safari zao na kwenda moja kwa moja kwa usafiri wa ndege ndani ya hifadhi hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari wanaotembelea hifadhi hiyo leo Mei 17, 2024, Ofisa Uhifadhi daraja la pili, Fatuma Mcharazo amesema kwa miezi 10 kutoka Julai 2023 hadi Aprili mwaka huu, wamepokea watalii 111,564 kati yao wageni wa nje ni 59,840 na Watanzania ni 51,724.

“Hii ni tofauti na miaka  ya nyuma, tulikuwa tunapokea watalii wengi wa ndani na wa nje wakiwa wachache, mfano mwaka 2020/2021 tulipokea watalii 46,517, raia wa kigeni wakiwa 15,104 pekee na mwaka 2021/2022 tulipokea watalii 66,890 huku wageni wakiwa 23,300  na mwaka 2022/ 2023 tulipata  109,112,  ambapo watalii kutoka nje walikuwa 50,133,” amesema Fatuma.

 “Kukua kwa utalii wa Zanzibar kumesaidia sana kusukuma maendeleo ya utalii katika hifadhi yetu, wengi wanaotembelea hapa wanatokea Zanzibar na hutua hapa kwa ndege na baada ya kumaliza shughuli zao hurudi Zanzibar,” amesema Fatuma.

Amesema miongoni mwa vitu vinavyowavutia watalii hao ni uwezo wa kuzunguka kufanya utalii katika mbuga hiyo yenye ukubwa wa Kilomita 3,230 kwa siku moja pekee na kuimaliza, huku wakiwa wameshuhudia wanyama wote muhimu.

Amesema katika kuhakikisha wageni hao wanavutiwa zaidi kubaki hifadhini  wanaanza mikakati ya kuongeza miundombinu ya malazi kutoka kulaza watalii 300 iliyopo sasa hadi kufikia watalii 600 kwa wakati mmoja.

“Mbali na hilo tunahakikisha uwanja wetu wa ndege wa Kikoboga unamalizika haraka ili kuweza kupokea ndege kubwa zaidi yenye uwezo wa kubeba hadi abiria 50 tofauti na sasa zinazotua ni za abiria 12,” amesema.

Mmoja wa waongoza watalii katika hifadhi hiyo, Joseph Chuwa ameiomba Serikali kusimamia kazi ya ujenzi wa uwanja wa Ndege Kikoboga ili ukamilike kwa haraka.

“Uwanja uliopo sasa ni mdogo, Serikali ingefanya mpango wa kuharakisha huu uwanja mkubwa wa ndege ulioanza kujengwa mwaka jana chini ya mradi wa Regrow,” amesema Chuwa.