Sheikh alia na wapigaji ripoti ya CAG

Sheikh wa Mkoa wa Pwani, Khamisi Mtupa akizungumza akiwa ofisini kwake. Picha na mtandao
Muktasari:
- Sheikh wa Mkoa wa Pwani ameeleza kukerwa na watumishi wa umma wanaohusishwa na ubadhirifu wa mali za umma katika ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG).
Kibaha. Sheikh wa Mkoa wa Pwani, Khamisi Mtupa amesema watumishi wa umma waliohusishwa na ubadhirifu wa fedha za umma katika ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG) wanarudisha nyuma juhudi za maendeleo ya nchi.
Mtupa ametoa kauli hiyo leo Jumamosi April 22, 2023 muda mfupi baada ya swala ya Iddi iliyofanyika mjini, akisema watu hao wamekosa uzalendo wan chi.
"Imefika mahali fedha nyingi zinatumika na wachache huku Watanzania wanendelea kutaabika jambo ambalo halipendezi hata machoni mwa Mungu na hali hii ikifumbiwa macho itaendelea kurudisha nyuma maendeleo," amesema
Amesema kuwa ili Tanzania iendelee na watu wake kuwa na ustawi, kuna umuhimu wa watu wanaopewa dhamana ya kusimamia miradi ya maendeleo kufanya kazi kwa hofu ya Mungu na si kutanguliza tamaa zao.
Pia amewanyooshea kidole baadhi ya walimu wa Shule za Msingi na vituo vya dini wanaotoa mafundisho yenye maadili yasiyozingatia tamaduni za nchi na kueleza kuwa wanajipalia makaa ya moto.
Mmoja wa waumini katika msikiti huo, Juma Bashara amesema kuwa ili Tanzania iendelee kupiga hatua katika nyanja mbalimbali kuna umuhimu wa kufanya tathmini ya watendaji walioko Serikalini na kuchukua hatua kwa wote wanaokwenda kinyume na sheria za utumishi wa umma.
"Serikali isendelee kuwakumbatia watumishi walioonyesha kukosa maadili kwa kula pesa za umma wafikishwe mahakamani na wakibanika adhabu iwapate," amesema
Naye Swaumu Shabani amesema kuwa Tanzania ina utajiri mkubwa na Iwapo watumishi wa umma watakuwa wazalendo hakutakuwa na shida.