Serikali yawapa magari ya kisasa Polisi, IGP Wambura asema...

Dar es Salaam. Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) Camillus Wambura amemshukuru Amiri Jeshi Mkuu, Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa magari mapya na ya kisasa kwa ajili ya matumizi ya operesheni mbalimbali za jeshi hilo.
IGP Wambura ametoa pongezi hizo leo Jumatatu, Aprili 28, 2025, jijini Dar es Salaam alipofanya ukaguzi wa magari hayo mapya, akisema yatasaidia kwa kiasi kikubwa kuongeza ufanisi wa kazi za Polisi katika maeneo mbalimbali ya nchi.

"Tunamshukuru sana Amiri Jeshi Mkuu kwa kutupatia magari haya ya kisasa. Yatarahisisha sana operesheni zetu na kuimarisha utendaji kazi wa Jeshi la Polisi kwa ujumla," amesema Wambura.
Aidha, IGP Wambura amewataka askari polisi wote kuendelea kufanya kazi kwa bidii, weledi, utii na uadilifu mkubwa, akisisitiza kuwa maboresho yanayofanywa na Serikali yanapaswa kuendana na ufanisi katika kutoa huduma bora kwa wananchi.

Amesema tangu Rais Samia aingie madarakani, Jeshi la Polisi limepata maboresho makubwa katika maeneo mbalimbali ikiwamo miundombinu, vifaa na mafunzo, hatua iliyosaidia kulifanya kuwa la kisasa na lenye weledi mkubwa katika kutekeleza majukumu yake ya kila siku.

"Tunaiona dhamira njema ya Mheshimiwa Rais kwa Jeshi la Polisi. Sasa ni wajibu wetu kuhakikisha tunaitikia kwa utendaji uliotukuka," amesema.