Mradi wa USAID kusaidia vijana 45,000 Zanzibar, Dar na Morogoro

Muktasari:
- Dk Tuhuma Tulli amesema mradi wa USAID kijana hodari unatarajia kuwawezesha zaidi ya vijana 45,000 ambapo 15,000 wa Zanzibar na 30,000 kutoka mikoa ya Dar es Salaam na Morogoro
Dodoma. Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye ulemavu, Patrobas Katambi amezindua mradi maalumu wa vijana ujulikanao kwa jina la USAID kijana Nahodha huku akiwataka vijana kujitambua.
Mradi huo unatekelezwa na Shirika la T MARC Tanzania kwa kushirikiana na mashirika ya Care International Tanzania, Youth Development Labs na Tanzania Youth.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Katambi amesema Serikali kupitia programu mbalimbali imekuwa ikiwawezesha vijana kupitia mfuko wa maendeleo ya vijana unaolenga kutoa mikopo nafuu kwa vijana ili kuendeleza shughuli za uzalishaji mali.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa mradi Dk Tuhuma Tulli amesema mradi huo unatarajiwa kutekelezwa kwenye mikoa miwili ya Tanzania Bara, Dar es Salaam na Morogoro pamoja na mikoa yote mitano ya Zanzibar.
Amesema mradi huo wenye thaman ya dola 10.6 milioni za Kimarekani unatarajia kuwawezesha vijana zaidi ya 45,000 ambapo 15,000 wa Zanzibar na 30,000 kutoka mikoa ya Dar es Salaam na Morogoro.
"Vijana wa Kitanzania wenye umri wa miaka 15-25, wana matumaini kuhusu mustakabali wao katika nchi ambayo hivi karibuni ilipata hadhi ya uchumi wa kati na ni moja ya nchi zinazokua kwa kasi kuchumi barani Afrika,” amesema Dk Tulli
Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID), Kate Somvongsiri amesema kwa kushirikisha vijana kwenye mipango ya kimaendeleo Tanzania ina nafasi nzuri ya kuunda na kutetekeleza miradi itakayotatua changamoto zinazozikabili ulimwengu.