Mawaziri wa afya wa EAC wakubaliana hatua za haraka kuikabili Ebola
Picha na Mtandao.
Muktasari:
- Baraza la mawaziri wa afya wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) limekubaliana kuoanisha ufuatiliaji wa ugonjwa wa Ebola na hatua za kinga katika viwanja vyote vya ndege, bandari na maeneo yote ya mipakani katika ukanda huo.
Arusha. Baraza la mawaziri wa afya wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) limekubaliana kuoanisha ufuatiliaji wa ugonjwa wa Ebola na hatua za kinga katika viwanja vyote vya ndege, bandari na maeneo yote ya mipakani katika ukanda huo.
Pia, wamekubaliana kuanzisha kikosi Kazi maalum cha kijeshi cha kikanda ili kuratibu mlipuko unaoendelea wa virusi vya Ebola (EVD).
Taarifa ya EAC kwa vyombo vya habari iliyotolewa leo Alhamisi, Juni 4, 2026 imeeleza hayo ni miongoni mwa maazimio makuu yaliyofikiwa katika mkutano wa nane wa dharura wa baraza la kisekta la mawaziri wa afya wa EAC, uliofanyika kwa njia ya mtandao Juni 1 hadi 2, 2026.
“Ili kuimarisha uzuiaji wa maambukizi ya mipakani, mawaziri walikubaliana juu ya haja ya kusawazisha ufuatiliaji wa Ebola na hatua za kinga kwenye viwanja vya ndege, bandari na vivuko vya mipakani katika nchi wanachama za EAC,” imeeleza taarifa hiyo.
Waliziagiza nchi wanachama kutekeleza hatua za ufuatiliaji na udhibiti katika maeneo yaliyoathirika, maeneo ya kuingilia, na mipaka isiyo rasmi kwa mujibu wa kanuni za kitaifa na mwongozo wa Shirika la Afya Duniani,” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.
Mawaziri walielekeza zaidi Sekretarieti ya EAC, ikifanya kazi kwa karibu na Wakala wa Usimamizi wa Usalama na Kinga wa Usafiri wa Anga wa Kiraia (Cassoa) na mashirika mengine husika, kuitisha haraka mkutano wa kikanda ili kusawazisha taratibu za uchunguzi, mahitaji ya tamko la afya la wasafiri na hatua nyingine za afya ya jamii katika maeneo ya kuingilia.
Pia mawaziri waliziagiza sekretarieti na nchi wanachama kuanzisha hatua za uchunguzi wa kutoka katika maeneo maalumu ya kuingilia kulingana na miongozo ya afya ya jamii ya kikanda na kimataifa.
Hata hivyo, sekretarieti ilielekezwa kuhamasisha rasilimali ili kusaidia uchunguzi ulioimarishwa, hatua za maji, usafi wa mazingira na usafi wa kibinafsi (WASH), mawasiliano ya hatari na ushirikishwaji wa jamii, na ufuatiliaji wa ugonjwa unaofanywa na jamii kote kikanda.
Katika hatua kubwa kuelekea kuimarisha uratibu wa kikanda, mawaziri walikubaliana kuanzisha kikosi kazi cha kikanda cha ufundi cha EAC kuhusu mshituko wa Ebola na magonjwa mengine yenye madhara makubwa.
Kikosi Kazi hicho kitajumuisha wataalamu walioteuliwa na nchi wanachama na sekretarieti ya EAC na kitakuwa na jukumu la kufuatilia mlipuko huo, kuratibu hatua za kiufundi, kupitia mienendo ya kidaktari ya ugonjwa na kutoa ripoti za mara kwa mara kwa mawaziri na vyombo vingine vya kisera vya EAC.
Nchi Wanachama za EAC zilielekezwa kuteua wataalamu wawili wa kiufundi kutoka wizara zao za afya na mtaalamu mmoja kutoka wizara zinazohusika na masuala ya EAC ili kuhudumu katika kikosi kazi hicho.
“Mawaziri pia walisisitiza umuhimu wa kubadilishana habari za kidaktari za ugonjwa kwa wakati halisi miongoni mwa nchi wanachama, ili kurahisisha ugunduzi wa mapema wa wagonjwa na kusaidia mshituko ulioratibiwa wa kikanda,” imeongeza taarifa hiyo.
Hadi kufikia Juni Mosi 2026, DRC ilikuwa imeripoti wagonjwa 121 waliothibitishwa na wagonjwa 1,077 wanaoshukiwa kuwa na virusi vya Ebola vya Bundibugyo, ikiwa ni pamoja na vifo 17 miongoni mwa wagonjwa waliothibitishwa na vifo 246 miongoni mwa wagonjwa wanaoshukiwa.
Uganda ilikuwa imeripoti wagonjwa 11 waliothibitishwa huku kukiwa na kifo kimoja kilichorekodiwa. Jumla ya watu 642 waliogusana na wagonjwa walikuwa wametambuliwa ambapo 638 kati yao walikuwa chini ya ufuatiliaji wa karibu, jambo linaloonyesha hatari zinazoendelea za maambukizi na haja ya kuimarisha uratibu wa mipakani.
Ili kuimarisha ufuatiliaji wa magonjwa na uwezo wa maabara, mawaziri waliziagiza nchi wanachama kuwezesha na kudumisha usambazaji wa maabara zinazotembea za EAC (mobile laboratories) na wataalamu wa kiufundi katika maeneo ya kimkakati, ikiwa ni pamoja na maeneo ya kuingilia mipakani na maeneo yaliyobainika kuwa hatarishi.
Mawaziri pia waliagiza sekretarieti ya EAC kuhamasisha rasilimali za ziada za kifedha na kiufundi ili kusaidia shughuli za ufuatiliaji na mshituko, na kuharakisha ununuzi na usambazaji wa maabara za makontena kote.
Maabara hizo zinazotembea za EAC zilitolewa kwa nchi wanachama chini ya mradi wa mtandao wa kikanda wa maabara za marejeleo wa EAC unaofadhiliwa na serikali ya Ujerumani kupitia Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KFW), na kwa usaidizi wa kiufundi kutoka Taasisi ya Bernhard Nocht ya Tiba ya Tropiki (BNITM), ambayo ni taasisi kubwa zaidi nchini Ujerumani kwa ajili ya utafiti, ufundishaji, ushauri, na matunzo katika nyanja ya magonjwa ya kitropiki na magonjwa ya kuambukiza yanayoibuka.
Mkutano huo ulibaini kuwa maabara kumi zinazotembea za EAC tayari zimeshasambazwa katika ukanda huo ikiwa ni pamoja na DRC, Uganda, Kenya, Rwanda, Burundi, Sudan Kusini, na Tanzania, ili kusaidia upimaji wa haraka na ugunduzi wa wagonjwa wanaoshukiwa kuwa na Ebola.
Mawaziri walipendekeza ununuzi wa vifaa vya kupimia Ebola na walisisitiza haja ya uwekezaji endelevu katika mifumo ya maabara inayoweza kugundua haraka vitisho vya magonjwa yanayoibuka mara kwa mara.