Kaya zaidi ya 28,000 zakabiliwa na upungufu wa chakula Monduli

Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la  CORDs, Yohana Ordorop akiongoza ugawaji mahindi ya msaada Monduli. Picha Mussa Juma

Muktasari:

Kaya 553 za wilaya ya Monduli, Mkoa wa Arusha zimepewa msaada wa mahindi tani 12 ili kukabiliana na njaa kutokana na uhaba mkubwa wa chakula ulitokana na ukame.

Monduli. Kaya 553 za wilaya ya Monduli, Mkoa wa Arusha zimepewa msaada wa mahindi tani 12 ili kukabiliana na njaa kutokana na uhaba mkubwa wa chakula ulitokana na ukame.

Afisa Miradi wa Shirika la Utafiti, Maendeleo na Huduma kwa Jamii (CORDs), Martha Katua akizungumza wakati wa kugawa chakula hicho, jana Jumamosi, Desemba 3, 2022 alisema shirika hilo limetoa msaada huo baada ya kubaini kaya nyingi zinakabiliwa na uhaba wa chakula.

Katau alisema wamegawa tani 12 za mahindi kwa kaya 553 katika Kata ya Mfereji Wilaya ya Monduli ambayo ipo pembezoni mwa wilaya hiyo.

Alisema vijiji ambavyo vimenufaika na msaada huo ni Indonyonodo ambacho kimepatiwa tani 6.5 kwa kugawanywa kwa Kaya 301 na Kijiji cha  Amalua Kaya 252  zimepata tani 5.5 za mahindi.

Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Indonyonodo wilaya ya Monduli wakiwa katika foleni ya kupata msaada wa mahindi kukabiliana na njaaa. Picha Mussa Juma

"Katika jamii hizi ambazo zinategemea ufugaji kuna uhaba mkubwa wa chakula kwani zinategemea kuuza mifugo ili kupata chakula lakini sasa mifugo mingi imekufa kwa ukame," alisema

Kwa upande wake, Kaimu Afisa Kilimo, wilaya ya Monduli Theobald Ngobya alisema wilaya hiyo inahitahi tani 28,000 za chakula.


Ngobya alisema kumekuwepo na uzalishaji mdogo wa chakula kwa misimu zaidi ya kiwili mfululizo katika wilaya hiyo hatua ambayo imesababisha upungufu wa chakula.

Alisema wilaya hiyo inaupungufu wa mahindi tani 22,550 na maharagr Tani 7578 ili kupunguza tatizo la uhaba wa chakula katika maeneo mengi.

"Msimu uliopita tulizalisha tani 5,639 za mahindi na tani 1,337 tu kiasi ambacho ni kidogo," alisema

Baadhi ya wanufaika wa msaada huo, Samweli Lonina na Neema Peter walishukuru CORDs kwa msaada wa mahindi ambao unaokoa maisha yao.

Lonina alisema wanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula hasa kutokana na ukame huku Neema akisema hivi sasa hata maziwa hawapati kwani mifugo mingi imekufa na mingine imedhoofika kwa kukosa malisho.

"Tunaomba Serikali na wadau wengine watusaidie chakula kwani licha ya kupata msaada huu bado tuna uhaba wa chakula," amesema.