Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Bashungwa aja na muarobaini wadaiwa sugu TBA

Muktasari:

  • Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa, ameuagiza Wakala wa Majengo (TBA), kuhakikisha unakusanya deni la Sh81.5 bilioni wanazodai kwa wapangaji wao, sambamba na kuwaondoa wadaiwa sugu katika nyumba hizo ili upatikanaji wa fedha hizo uweze kusaidia utekelezaji wa miradi mingine nchini.

Dodoma. Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa, ameuagiza Wakala wa Majengo (TBA), kuhakikisha unakusanya deni la Sh81.5 bilioni wanazodai kwa wapangaji wao, sambamba na kuwaondoa wadaiwa sugu katika nyumba hizo ili upatikanaji wa fedha hizo uweze kusaidia utekelezaji wa miradi mingine nchini.

Ameyasema hayo leo Septemba 07, 2023 jijini Dodoma, alipofanya ziara yake kwa mara ya kwanza, kwenye ofisi za Wakala huo na kuzungumza na menejimenti ya TBA ambapo amesisitiza juu ya uwekezaji wenye tija kwa watumishi na Taifa kwa ujumla.

“TBA simamieni sheria, kwa yeyote asiyelipa kodi hata kama ni kiongozi, waandikieni notisi ya kulipa madeni yao na wasipolipa waondoeeni, wapo wengine nje wanasubiri wapewe nyumba ili waweze kulipa kodi kwa wakati na tutatumia makusanya hayo kujenga nyumba nyingine,” amesisitiza Bashungwa.

Aidha, Bashungwa ameagiza TBA kuhakikisha wanakuja na mikakati itakayosaidia kujenga nyumba za bei nafuu hasa kwa vijana wanaoajiriwa katika utumishi wa umma hususan Dodoma, ili kuweza kumudu gharama za maisha.

“Kuna vijana ambao wanaingia kwenye kada ya utumishi wa umma na bado hawajawa na uwezo wa kujijengea nyumba, kupitia TBA mnaweza kujenga nyumba za bei rahisi kwa ajili ya vijana hao ili kuwarahisishia gharama za Maisha,” amesema waziri huyo kijana.

Aidha, ameutaka wakala huo kuwa na utaratibu wa kuwajengea uwezo wataalamu walionao ili kuenda sambamba na kasi ya mabadiliko ya teknolojia hasa katika suala la ujenzi na uendelezaji wa majengo mbalimbali.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa TBA, Daud Kondoro, amesema kuwa wakala huo utahakikisha unatafuta ufumbuzi wa changamoto zilizopo na kumuahidi wazir huyo, kuandaa mikakati mizuri itakayosaidia TBA kutoa huduma bora kwa wananchi.

Awali, bosi huyo wa TBA ameeleza namna ambavyo taasisis yake inaendelea kutekeleza mradi wa ujenzi wa nyumba 3500 za watumishi wa umma eneo la Nzuguni Dodoma, ambapo awamu ya kwanza ya nyumba 150 utekelezaji umefikia asilimia 95 na awamu ya pili ya ujenzi wa nyumba 150 utekelezaji wake umefikia asilimia 10.

Miradi mingine kwa mujibu wa Kandoro ni pamoja na ujenzi wa nyumba 20 za viongozi jijini Dodoma, ambazo zililenga kukabiliana na uhaba wa nyumba za viongozi baada ya Serikali kuhamia Dodoma ambapo mradi huo umekamilika kwa asilimia 100 na nyumba zimeanza kutumiwa na Viongozi.

Waziri Bashungwa anaendelea na ziara yake ya kutemebelea taasisi zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi.