Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Pasaka na simulizi zake

Mchoro unaonyesha sehemu ambayo Yesu alizikwa kisha kukufuka.  Picha na Maktaba

Wakristo  duniani kote wanajiandaa kusherehekea Sikukuu ya Pasaka. Ingawa si madhehebu yote ya Kikristo yanayosheherehea kwa uzito sawa, katika kalenda ya Kanisa Katoliki, Pasaka ni furaha ya kusherehekea kufufuka kwa Yesu.

Ijumaa Kuu
Ijumaa Kuu ni siku ambayo wakristo wanaadhimisha kufa, kuzikwa kwa Yesu, tukio lililotokea katika mji wa Yerusalemu siku ya Ijumaa.

Kulingana na Mtume Yohane, kesho yake, yaani baada ya Ijumaa, ilikuwa Sabato na ikafuatia na Pasaka yenyewe siku ya Jumapili. Ijumaa Kuu ni sehemu ya Juma Kuu linaloanza kwa adhimisho la Yesu kuingia mji huo wa Yerusalemu akishangiliwa kama mfalme wa Wayahudi. Ijumaa Kuu pia ni sehemu ya siku tatu kuu za Pasaka zinazoadhimisha mateso na kifo chake, kuzikwa kaburini, na hatimaye kufufuka.

Simulizi za malaika
Siku moja malaika alimtokea binadamu na kumuuliza “Ni kitu gani unataka nikufanyie?”. Wakati binadamu anafikiria jibu, malaika akampa tahadhari, akamwambia “ Lakini chochote utakachoomba nikufanyie, jirani yako atapata mara mbili”. Ulikuwa ni mtihani mkubwa sana kwa binadamu.

Kwa maisha ya kawaida huwezi kuelewa malaika alikuwa anampima nini binadamu. Na binadamu hakujua kuwa malaika alitumwa na Mungu na Mungu alikuwa anajua nafsi ya binadamu, na hicho kilikuwa kielelezo cha binadamu wengi hasa kwa maisha ya sasa hivi.

Binadamu alitafakari sana, alifikiri, nikiomba nyumba, jirani yangu atapata mbili, nikiomba gari atapata mbili, nikiomba fedha atapata mara mbili. Mwisho akapata jibu, tena bila wasiwasi akamwambia malaika, nitoboe jicho moja. Alifahamu kuwa akitobolewa jicho moja, jirani atatobolewa macho yote mawili.

Maisha yetu ndivyo yalivyo. Tutasoma neno la Mungu, tutahudhuria kanisani, tutashiriki katika semina za neno la Mungu yote yatapita, upendo kama nguzo ya imani inapotea na itaendelea kupotea daima kama hatutabadilika.

Umuhimu wa Pasaka
Pasaka ni moja ya sikukuu kubwa sana kwa Wakristo. Pamoja na kuwa imeendelea kuchukuliwa kama tukio la kihistoria tu, bado dhana yake ya kuonyesha upendo wa Mungu kwa wanadamu haitapotea. Ni upendo wa kutoa moja ya nafsi za Mungu, iteswe, isulubiwe, ife na kisha ifufuke kudhihirisha utukufu wa Mungu na upendo wake kwa wanadamu.

Lakini kwa sisi wanadamu wa leo Pasaka ni nini?
Kuna umuhimu gani wa kuendelea kukumbuka Sikukuu ya Pasaka? Ni mafundisho gani tunayoyapata juu ya siku hii? Pasaka ni sikukuu ya kufufuka kwa Yesu Kristo na ni sikukuu muhimu kwa Wakristo, watu huenda kanisani na kusherekea sikukuu hii ya kidini.

Simulizi zaidi
Hadithi au habari za Pasaka zinatoka katika kitabu kitukufu, Biblia. Injili inasema kuwa mwili wa Yesu Kristo ulitoweka kutoka katika kaburi lake katika siku ya tatu baada ya kusulubiwa kwake msalabani.Malaika waliwatokea wafuasi wake na kuwaeleza kuwa Yesu amefufuka.

Wakristo pote ulimwenguni husherekea Pasaka kwa furaha kubwa sana kwa sababu wanaiona ndio siku ambayo mwokozi wao huwa amefufuka. Watu wengi huvalia nguo mpya kwenda kanisani siku ya Pasaka.

Kuna alama nyingi zinazotambulisha siku ya Pasaka, moja ni msalaba ambao Wakristo, huuona kama alama ya ushindi wa Kristo dhidi ya kifo. Msalaba mara nyingi hutokea kama alama ya Pasaka. Watu katika sehemu nyingi ya ulimwengu huoka keki maalumu ziitwazo ‘mikate ya moto ya msalaba’.

Wagiriki na Wareno hula mkate maalumu wa duara uliookwa na kutiwa alama ya msalaba na kupambwa na mayai ya Pasaka.

Mapambo ya Pasaka na picha za kuchora mara nyingi hujumuisha umbo la mwanakondoo kama alama ya Yesu kristo.

Mwanakondoo ni moja ya chakula cha asili cha Pasaka, na mapishi na keki zenye maumbo kama ya mwanakondoo hupamba mezani wakati wa Pasaka kwa baadhi ya familia.
Alama ya mwanakondoo inatokana na sherehe za Wayahudi ya Pasaka au ‘pass over” Wayahudi walimtoa mwanakondoo kama dhabihu iitwayo ‘Mwanakondoo wa Pasaka’ wakati wa kipindi chao cha asili cha sherehe za Pasaka katika hekalu za Yerusalemu.

Wakristo wa awali walichukulia toleo la dhabihu ya mwanakondoo kama tabirio la kusulubiwa kwa Kristo msalabani. Walimwelezea Yesu Kristo kama mwanakondoo wa Mungu ambaye amechukua dhambi za ulimwengu.

Mishumaa na mengineyo
Taa, mishumaa na moto mkubwa wa sherehe inatoa ishara ya kusherekea kwa Pasaka katika baadhi ya nchi.

Wakatoliki katika baadhi ya nchi huzima taa zote katika makanisa yao siku ya Ijumaa kuu. Jioni ya siku inayotangulia Pasaka, hutengeneza moto mpya kuwashia mshumaa mkubwa wa Pasaka kuashiria siku na mambo mapya ndani ya ufufuo mpya wa Yesu.

Hutumia mshumaa huu kuwashia mishumaa mingine yote kanisani. Halafu huwasha mishumaa yao nyumbani ili itumike katika nyakati za sherehe maalumu.

Katika sehemu za Ulaya Kaskazini na Kati,watu huchoma moto mkubwa wa sherehe katika vilele vya milima. Halafu hujikusanya kuzunguka huo moto mkubwa na kuimba nyimbo na mashairi ya Pasaka.

Mwanzo wa Pasaka
Wakristo hufanya ibada ya siku 40; kipindi cha mfungo na sala hujulikana kama Kwaresma.Inakumbusha siku 40 za Kristo kufunga na kwenda jangwani.

Wiki ya mwisho ya Kwaresma iitwayo wiki takatifu hutukuza matukio ya wiki ya mwisho wa maisha ya Yesu Kristo kuwepo duniani, na inaanza katika Jumapili ya Matawi. Imetajwa hivyo kwa sababu ya matawi ambayo watu waliyatawanya kabla Yesu kristo hajaingia Yerusalemu kwa kushangiliwa kwa shangwe kubwa.

Katika Alhamisi ya wiki ya mwisho ya Kwaresma kabla ya Ijumaa Kuu, Wakristo hukumbuka chakula cha mwisho cha Yesu Kristo cha jioni wakati walipoosha nyayo za miguu yao.

Waliiona Ijumaa Kuu ya kusulubiwa kwa Yesu kristo katika namna au njia ya huzuni na majonzi na kutumia Jumamosi takatifu katika fikra ya mambo yatakayotokea mbeleni katika Jumapili ya Pasaka.