Mzee Onyango afariki dunia, chanzo chatajwa
Mwigizaji mkongwe wa filamu nchini, Issa Joseph maarufu kwa jina la Mzee Onyango enzi za uhai wake. Picha na Mtandao
Muktasari:
- Taarifa za kifo chake zimethibitishwa na mtoto wake, Joseph Issa, ambaye amesema baba yake alifariki majira ya saa saba usiku baada ya kusumbuliwa na ugonjwa wa shinikizo la damu (presha) kwa muda mrefu.
Dar es Salaam. Mwigizaji mkongwe wa filamu nchini, Issa Joseph maarufu kwa jina la Mzee Onyango, amefariki dunia usiku wa kuamkia leo katika Hospitali ya Jeshi ya Lugalo, jijini Dar es Salaam.
Taarifa za kifo chake zimethibitishwa na mtoto wake, Joseph Issa, ambaye amesema baba yake alifariki majira ya saa saba usiku baada ya kusumbuliwa na ugonjwa wa shinikizo la damu (presha) kwa muda mrefu.
Joseph amesema baba yake alikuwa akipata nafuu mara kwa mara licha ya kuendelea kuugua ugonjwa huo kwa kipindi kirefu.
"Mzee alikuwa anasumbuliwa na presha kwa muda mrefu. Wakati mwingine hali yake ilikuwa inaimarika na wakati mwingine kurudi tena kuwa mbaya. Safari hii ugonjwa umejitokeza kwa nguvu zaidi na hatimaye kusababisha kifo chake.
"Mimi bado niko njiani natokea Dodoma. Taratibu za mazishi bado hazijapangwa. Familia ikikamilisha maaandalizi, taarifa zaidi zitatolewa kwa umma," amesema.
Kwa mujibu wa familia, msiba upo Kawe Triple Seven jijini Dar es Salaam ambako ndugu, jamaa na marafiki wameanza kufika na kutoa pole.
Enzi za uhai wake Mzee Onyango ameonekana katika filamu na tamthilia mbalimbali ikiwemo, Babu The Perfect Man, Ripoti, Kimbembe na nyinginezo.