Mume wa aliyeimba 'Ekwueme' ahukumiwa kunyongwa hadi kufa

Muktasari:
- Jaji Njideka Nwosu-Iheme ametoa hukumu hiyo jana Jumatatu, baada ya Peter kukutwa na hatia ya kufanya mauaji ya mkewe kwa kukusudia Aprili 8, 2022.
Nigeria. Mahakama ya Juu ya Wilaya ya Shirikisho iliyopo Wuse Zone 2, Abuja imemuhukumu kunyongwa hadi kufa, Peter Nwachukwu, ambaye alikuwa mume wa mwimbaji maarufu wa nyimbo za injili, Osinachi Nwachukwu.
Jaji Njideka Nwosu-Iheme ametoa hukumu hiyo jana Jumatatu, baada ya Peter kukutwa na hatia ya kufanya mauaji ya mkewe kwa kukusudia Aprili 8, 2022.

Utakumbuka Peter alikuwa akikabiliwa na mashitaka 23 ikiwemo mauaji kwa kukusudia, unyanyasaji kwa mke wake, ukatili kwa watoto na vitisho vya kihalifu. Hata hivyo wakati wa kesi hiyo, upande wa mashtaka walipele mashahidi 17, wakiwemo watoto wawili wa marehemu, na kuwasilisha vielelezo 25.

Katika hukumu yake, Jaji Nwosu-Iheme alisema upande wa mashtaka umeweza kuthibitisha kesi yake pasipo shaka yoyote. Aidha baada ya maombi ya kupunguzwa adhabu kutoka kwa wakili wa Nwachukwu, Reginald Nwali, mahakama ilimhukumu adhabu ya kifo kwa kunyongwa kwa kosa la kwanza ambalo ni mauaji.
Pia alihukumiwa kifungo cha ziada cha kati ya miezi sita hadi miaka mitatu kwa mashitaka mengine kadhaa na kulipa faini ya N700,000.

Ikumbukwe Osinachi alifariki dunia Aprili 8, 2022, akiwa na umri wa miaka 42. Enzi za uhai wake wengi walimfahamu zaidi kuanzia mwaka 2017 alipoimba wimbo wake 'Ekwueme'