Gilmour alia kukosa Kombe la Dunia
Kiungo wa Scotland, Billy Gilmour. Picha na Mtandao
Muktasari:
- Gilmour amesema kukosa Kombe la Dunia ni jambo ambalo litamtesa kichwani kwa muda mrefu.
Kiungo wa Scotland, Billy Gilmour, amesema kuwa atachukua muda kukubaliana na maumivu ya kukosa Kombe la Dunia baada ya kuondolewa kwenye kikosi kitakachoshiriki mashindano hayo kutokana na majeraha.
Gilmour alilazimika kutolewa uwanjani akiwa na jeraha la goti katika kipindi cha kwanza cha mchezo ambao Scotland iliifunga Curacao mabao 4-1 kwenye Uwanja wa Hampden Jumamosi iliyopita, kabla ya timu kusafiri kwenda Marekani siku iliyofuata.
Nyota huyo wa Napoli mwenye umri wa miaka 24, alifanyiwa vipimo vya uchunguzi mara tu baada ya mechi hiyo na baadaye ilibainika hatoweza kucheza Kombe la Dunia mwaka huu huku nafasi yake ikichukuliwa na Tyler Fletcher.
Gilmour amesema kukosa Kombe la Dunia ni jambo ambalo litamtesa kichwani kwa muda mrefu.
“Ninakosa maneno ya kuelezea jinsi ninavyohisi kwa sasa.
“Kuwa karibu sana kutimiza ndoto yangu ya utotoni ya kucheza Kombe la Dunia, halafu ghafla nafasi hiyo imeondolewa kwangu kutokana na jeraha. Imekuwa hali ngumu sana kuikubali na kuielewa.
“Msaada wenu na jumbe zenu za faraja mlizonitumia katika siku chache zilizopita zina maana kubwa sana kwangu na sijazipuuzia, hivyo nawashukuru sana.
“Nitarejea hivi karibuni nikiendelea kufanya kile ninachokipenda, lakini hadi wakati huo, tuiunge mkono timu na tuishangilie. Twende Scotland,” alisema Gilmour.