Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Gamondi ageukia waliomtimua Sven

Muktasari:

  • Yanga wenye pointi 24 baada ya kushuka uwanjani mechi tisa, ikishinda nane na kupoteza moja dhidi ya Ihefu, imepangwa Kundi D katika michuano hiyo ya CAF sambamba na watetezi, Al Ahly ya Misri, CR Belouzdad ya Algeria na Medeama ya Ghana.

Dar es Salaam. Kocha wa Yanga, Miguel Gamondi amewaita mastaa wa timu hiyo kambini jana ili kuanza maandalizi ya mechi zijazo za kimataifa za Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya CR Belouzdad inayonolewa na Kocha mpya, Mbrazili Marcos Paqueta aliyechukua nafasi ya Sven Vandebroeck anayetajwa mitandaoni kwamba Simba wanamtamani.

Yanga yenye pointi 24 baada ya kushuka uwanjani mechi tisa, ikishinda nane na kupoteza moja dhidi ya Ihefu, imepangwa Kundi D katika michuano hiyo ya CAF sambamba na watetezi, Al Ahly ya Misri, CR Belouzdad ya Algeria na Medeama ya Ghana.

Timu hiyo itaanza mechi ya kwanza ugenini dhidi ya CR Belouzdad Novemba 24 kabla ya kuikaribisha Al Ahly katika mechi itakayofuata Desemba 2.

Gamondi aliyetua Yanga msimu huu kutoka Argentina aliiwezesha timu hiyo kutinga makundi baada ya kuzing’oa Asas ya Djibouti kwa jumla ya mabao 7-1 kisha kunyoa Al Merrikh ya Sudan kwa mabao 3-0 aliwapa mapumziko wachezaji baada ya kazi kubwa dhidi ya Simba na Coastal.

Yanga jana walifanya mazoezi asubuhi na kurudi majumbani kwao, Mwananchi imezungumza na Gamondi ambaye amekiri, licha ya mastaa wake kuwa na mwendelezo mzuri wa matokeo bado anahitaji kuendelea kuwaweka fiti ili kujihakikishia nafasi ya kucheza robo fainali.

“Ubora wa Yanga unatokana na kuwajibika kwa wachezaji wangu pia wamejengwa vizuri wamekuwa na utimamu wa mwili ukiangali tumekuwa bora vipindi vyote hayo ni majibu kwamba timu imekamilika na imejengwa vizuri,” alisema Gamondi na kuongeza;

“Kuendelea kufanya mazoezi ni mpango mzuri kwetu kama benchi la ufundi waliopo wataendelea kufanya mazoezi wakitokea nyumbani mapumziko itakuwa ni siku za wikiendi tu.”

Alisema ubora wa kikosi chake unatokana na mambo mengi huku akitaja kuwajibika kwa kila mmoja kuwa ndio siri kubwa ya mafanikio waliyonayo.

“Yanga kuanzia benchi la ufundi, wachezaji na viongozi tumekuwa wamoja hii ni njia bora na ya kujenga pamoja ili kuweza kufikia mafanikio jambo ambalo hadi tulipofikia sasa tunaona mwanga,” alisema Gamondi na kuongeza;

“Akili yote sasa imehamia kimataifa tunataka kuweka rekodi nyingine baada ya kutinga hatua ya makundi baada ya miaka 25 malengo sasa ni kusonga mbele zaidi kwa kucheza robo fainali.”

Alisema wachezaji wanampa nguvu na moyo wa kuendelea kuwaweka fiti kutokana na juhudi zao kila wanapokutana mazoezini hakuna mchezaji anamuonyesha kuchoka wamekuwa na kasi, nguvu na upambanaji wakiamini hakuna kinachoshindikana. Yanga imetinga makundi ikiwa ni miaka 25 tangu ilipofika hatua hiyo kwa mara ya kwanza mwaka 1998, ikiwa ni miezi michache baada ya fainali ya Kombe la Shirikisho.