Dondoo za usajili EPL dirisha likikaribia kufungwa
Muktasari:
- Dirisha kubwa la usajili la majira ya kiangazi litafungwa leo saa 4:00 usiku kwa muda wa Afrika Mashariki.
Zimebakia saa zisizozidi tano kabla ya dirisha kubwa la usajili la majira ya kiangazi kwa timu za Ligi Kuu England (EPL) kufungwa.
Dirisha hili litafungwa leo Septemba Mosi, 2025 saa 4:00 usiku kwa muda wa Afrika Mashariki na baada ya hapo timu hazitokuwa na nafasi tena ya usajili wa wachezaji kutoka timu nyingine isipokuwa wale ambao watakuwa huru.
Wakati muda ukizidi kuyoyoma, siku ya leo kuna wachezaji ambao uhamisho wao umekamilika, wapo ambao wanakaribia kukamilisha na kuna wale ambao michakato ya uhamisho wao imekwama.
Jackson atua Bayern Munich
Hatimaye uhamisho wa mkopo wa Nicolas Jackson kutoka Chelsea kwenda Bayern Munich umekamilika.
Mchezaji huyo anajiunga kwa mkataba wa mkopo wa msimu mmoja wenye thamani ya Pauni 14.2 milioni ambao unamfanya aweke rekodi ya uhamisho ghali zaidi wa mkopo huku kukiwa na kipengele cha kumnunua jumla kwa Pauni 56.2 milioni.
Awali timu hizo zilikubaliana ila ghafla Chelsea wakataka mchezaji huyo abakie na sasa limefufuka upya na kukamilika.
Guehi na Liverpool
Liverpool inakaribia kumsajili beki wa Crystal Palace, Marc Guehi kwa uhamisho wa Pauni 35 milioni.
Guehi atasaini mkataba wa miaka mitano kuitumikia Liverpool ambayo inatetea ubingwa EPL.
Martinez aigomea Galatasaray
Kipa wa Aston Villa, Emiliano Martinez amekataa mpango wa timu yake kumuuza kwenda Galatasaray ya Uturuki.
Martinez amefunguliwa mlango wa kutokea na timu hiyo ambayo sasa kipa namba moja ni Marco Bizot.
West Ham yatoswa kwa Cresswell
West Ham imeshindwa kumshawishi Charlie Cresswell wa Toulouse kujiunga na timu hiyo ili azibe pengo la Nayef Aguerd.
Timu hiyo pia imeulizia uwezekano wa kumpata Axel Disasi wa Chelsea.
Edouard kutua Lens
Mshambuliaji wa Crystal Palace, Odsonne Edouard amesafiri kwenda Ufaransa kujiunga na Lens kwa uhamisho wa Pauni 3.2.
Sancho anyemelea Aston Villa
Aston Villa inahaha katika saa za majeruhi za dirisha kubwa la usajili kukamilisha uhamisho wa Jadon Sancho kutoka Manchester United.
Donnarumma kimeeleweka Man City
Manchester City itakamilisha leo uhamisho wa kipa Gianluigi Donnarumma kutoka PSG.
Koło Muani aibukia Spurs
Mshambuliaji wa Juventus, Randal Koło Muani amesafiri kwenda London, England kukamilisha usajili wa kujiunga na Tottenham Hotspur.