Azam yapata Mtendaji Mkuu Mpya akitokea Hispania
Muktasari:
- Kabla ya kuteuliwa kuwa Mtendaji Mkuu Msaidizi, Rashid Seif alikuwa sehemu ya benchi la ufundi la Azam FC.
Dar es Salaam. Octavi Anoro kutoka Hispania, ameteuliwa kuwa Mtendaji Mkuu wa Azam FC, uteuzi ambao umetangazwa leo rasmi na Klabu hiyo yenye makazi yake Chamazi, Dar es Salaam.
Taarifa ya Azam FC, imesema kuwa Octavi amepewa mkataba wa miaka miwili.
Mtendaji Mkuu wa Azam FC, Octavi Anoro
“Bodi ya Azam Football Club, inayo furaha kumtangaza, Octavi Anoro, (42), kama Mtendaji Mkuu (CEO) mpya wa klabu, kwa mkataba wa miaka miwili, hadi 2027.
“Nafasi hiyo ilikuwa wazi kufuatia aliyekuwa akiishikilia, Abdulkarim Nurdin maarufu kama Popat, kupandishwa cheo na kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais.
“Anoro, raia wa Hispania, anakuja na maarifa na uzoefu mkubwa wa kimataifa katika nyanja ya maendeleo ya utawala na biashara ya mpira wa miguu,” imefafanua Azam FC.
Mtendaji Mkuu Msaidizi, Rashid Seif
Timu hiyo imesema kuwa Anoro atakuwa akisaidiwa na Rashid Seif ambaye alikuwa miongoni mwa maofisa wake wa benchi la ufundi.
“Aidha, Bodi pia imemteua, Rashid Seif Mohamed, kuwa msaidizi wa Mtendaji Mkuu (Assistant CEO).
“Rashid ni mhitimu wa Shahada ya Umahiri ya utawala wa michezo (Master's in Sports Management) pamoja na ngazi ya pili ya ukocha kutoka chama cha soka cha England, FA.
“Uteuzi huu ni muendelezo wa harakati za klabu
kujipambanua kiweledi katika ukuaji wa kimkakati na kuweka alama muhimu kwenye mageuzi ya kiuongozi kwa ajili ya ustawi wa muda mrefu,” imesema Azam FC.