Chama atua Yanga, dili lake liko hivi

Muktasari:

  • Klabu ya Yanga imetangaza rasmi kuinasa saini kiungo mshambuliaji kutoka Simba, Clatous Chama

Dar es Salaam. Baada ya kumfukuzia zaidi ya miaka miwili nyuma hatimaye mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Bara, Yanga wamefanikiwa kuinasa saini ya kiungo mshambuliaji kutoka Simba, Clatous Chama.

Kiungo huyo ambaye amemaliza mkataba wake na Simba, Juni 30 na leo Julai Mosi ametambulishwa Jangwani kwa mkataba wa mwaka mmoja.

Kiungo huyo msimu ulioisha ameifungia Simba mabao saba ya Ligi Kuu Bara huku akitupia mabao matatu Ligi ya Mabingwa Afrika kutua kwake Yanga anaenda kuungana na Pacome Zouzoua, Maxi Nzegeli na Stephane Aziz Ki ambaye uongozi unapambana kumbakiza baada ya mkataba wake kumalizika.

Usajili wa kiungo huyo kukamilika umezima tetesi zilizokuwa zinazungumzwa kwa kumbakiza Simba huku wengine wakithibitisha kusajiliwa na Yanga kama ambavyo Mwananchi lilithibitisha.

Chama ni mzoefu wa Ligi Kuu Bara akiitumikia Simba kwa misimu sita na kuchangia mafanikio kama kutwaa mataji ya ndani na kuisaidia timu hiyo kucheza hatua ya robo fainali Ligi ya Mabingwa Afrika.

Kiungo huyo alitua Tanzania msimu 2018 aliitumikia timu hiyo hadi 2021 kabla ya kuuzwa RS Berkane ambayo aliitumikia kwa miezi sita tu na baadaye kurudi tena Simba hadi leo alipotambulishwa kujiunga na Yanga.