Prime
FYATU MFYATUZI: WaKi-Nyaa mkome kutaka ‘kutovuka na kutuvurugia’

Kwanza nikiri. Ukitaka kufyatuka na kufyatua wanaokufyatua, hakikisha hukosi kutumia zana za kileo hasa mtandao.
Hivyo, Fyatu Mfyatuzi nami ni geek au gwiji wa mtandao. Juzi, katika kupitia mitandao baada ya bi mkubwa kuchefukwa na kukinukisha, nilikuta matusi ya nguoni toka kwa mafyatu wa kaya jirani wakimtukana yeye na mafyatu wote. Nilishangaa, kuchukia, na kusikitika kiasi cha kuamua kufyatua hiki kitu ili wahusika wakome na kukomaa.
Naonya. Asitokee yeyote akaniita chawa awe wa baba au mama. Mie siyo wala sijawahi kuwa chawa. Mie ni Fyatu. Period.
Bi nkubwa ambaye kitaaluma ni doktari wa karibu kila kitu na mafyatu wote wananijua uzuri kuwa huwa siiti koleo kijiko kikubwa bali koleo. Huwa sitetei ujinga na uzwazwa. Nachukia jinai, ubabaishaji, ukandamizaji, hata usanii vifanywe kwa kisingizio chochote iwe amani, imani, siasa, au visasi.
Pili, baada ya bi nkubwa kumfyatua mtundu Tunda ambaye, kwa ‘utundu’ wake, anataka kutishia ulaji wake, kaya nzima ililipuka, kufyatuka, na kugawanyika pande mbili. Wanaounga ‘uzalendo’ na wanaoipinga. Kwani, hawajui kuwa Mtundu anasulumbiliwa na utundu tu na uharibifu? Maji yalizidi unga hadi kuvutia mafyatu jirani.
Kwanza, nafyatua hii kitu kuwaonya mafyatu wangu na bi nkubwa hawahitaji msaada wao kwa wanachodai ni haki za binadamu. Mafyatu ni mafyatu. Hawahitaji haki za binadamu bali kufyatuka ili wazisake wenyewe wajuavyo.
Pili, naonya dhahiri mambo ya Ngoswe aachiwe Ngoswe. Maza anashangaa. Lini walituona kwao tukienda kuwatetea kana kwamba hawana uwezo wa kujitetea kama sisi, sorry, kama wao? Unakwendaje kumsaidia fyatu ambaye hajakuomba msaada? Wapo wanaodai eti wanataka kutumia fursa hii kutanua ughaibuni wakisingizia kutetea mafyatu wa kaya yetu. Natoa angalizo na onyo. Hakuna haja kuchukiana au kudepotiana. Tuamke.
Tuache kutumiwa kama kichwa cha mwendawazimu walevi kujifunzia kunyoa. Tufyatuke na kujitetea. Tusingoje kutetewa au kufyatuliwa ndiyo tufyatuke.
Tatu, wafurukutwa wanahoji, kama tutakuwa wakweli, kuna lisirkal habithi kama la kwao?Fyatu mmoja aliuliza “je mbona hawajamaliza mtiti wa mauaji, utekaji, na upoteaji wa Gen Z? Au wanataka kuwafyatua Gen Ziro na mafyatu wetu wafyatuke na kuwafyatua watukufu walioletwa na Sir God mwenyewe? Mshindwe na kulegea hadi mlegelege. Hapa, naona ufyatu. Kama ni utekaji, upotezaji, na unyotoaji roho, upo kaya zote aliwahi kusema maza au hamkumuelewa? Mbona juzi alinyotolewa roho mwishiwa tena katikati ya jiji la Nairoberry mbali na kasisi aliyejenga usuhuba na mpingaji maarufu wa kwao aliyefyatuliwa.
Nani kashikwa? Kwanini? Hawa ‘viherehere’ wamefanya nini? Lazima waeleweshwe na waelewe. Kwetu ni amani tupu hata kama ni ya imani.
Hatujanyotoa roho ya mwishiwa yeyote. Kama ni kasisi, wetu alifanyiwa massage bila kunyotolewa roho sawa na kwao. Isitoshe, ‘tumeishawashika’ watuhumiwa.
Pia, wajue. Ndata wetu hawajadata kama wao. Hamkuona juzi, pale kwa pilato, walivyoonyesha amani na imani kiasi cha mafyatu kwenda kuchonga na Mtundu bila kupigwa, kutishwa, wala kuingizwa tunduni?
Nne, sikupenda walivyomuudhi bi nkubwa wetu kiasi cha kumlazimisha azoze. Sasa nasema. Mkome na kama mbaya mbaya msije kutovuka na kutuvurugia ulaji wetu.
Yenu yawashinda. Yetu yawahusuni? Leo, mwaja na gea ya kutetea wapingaji ambao ‘hawapendwi’ hata na chawa achilia mbali mafyatu.
Kesho, kwa vile huu ni mwaka wa uchakachuaji ambapo nimeishajihakikishia ushindi wa kishindo na miujiza, mtakuja kuhoji uchakachuaji wetu kana kwamba kwenyu hawachakachui na kuchakachuana kama ambavyo nasi tunafanya na ngoma inakuwa droo.
Tano, nimekasirika sana kwa watundu kumkasirisha bi nkubwa wetu mpendwa, mbeba maono, aliyefungua kaya na kutenda miujiza kiuchumi. Nadhani wanatuonea wivu. Haiwezekani waje kutufundisha namna ya kufyatuana hata kama tumegoma kufyatuka na kufyatua hao wanaotaka tuwafyatue. Haraka ya nini? Msituvurugie.
Wakati wa kufyatuka na kufyatua ukifika, wala hatutahitaji msaada wenyu wala tuisheni juu ya namna ya kufyatuka na kufyatua. Hata hivyom, wana bahati.
Ningekuwa mimi, ningewaweka tunduni kama yule Mtundu wakaishi naye kama wanampenda sana. Ebo! Tuheshimiane.
Iweje fyatu atake kukinukisha nao wamuunge mkono? Kikinuka kikanukishwa, si tutanuka wote?
Hata kama tunanuka tayari, nani anataka kuongezewa harufu mbaya baada ya kukinukisha? Isitoshe, tukinukishe au kutokinukisha, wao yawahusuni? Pilipili usizokula zakuwashani? Wasitake kujua kunguni wa kitanda wasicholalia.
Mwisho, nawajuza hawa ‘viherehere’ kuacha ‘kiherehere.’ Sisi, japo mafyatu, tumegoma kufyatuka hadi Mwana wa Maria arejee ndiyo tufyatuke na kwenda kutesa mbinguni.
Kama wanaona wivu namna bi nkubwa anavyoupiga mwingi, si waende awamegee maono nao watende miujiza ya kuzuia mafyatu wao kufyatuka na kukinukisha? Wanacheza na kukinukisha! Wanajua maana na madhara ya kukikunikisha?
Tuonane wiki ijayo.