Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

FYATU MFYATUZI: Marufuku mafyatu kugwijimisha religion na politics

Baada ya kushuhudia yaliyowakuta wenzetu kwenye kiama twawala, Fyatu Mfyatuzi nimestuka. Lazima nichukue hatua mujarabu bila huruma.

Kabla ya zari la mtiti wa fyatu kidhabu kujifyatua na kujifanya akitaka kutumikia mabwana wawili na kujigeuza msemaji wa kiama akafyatua yasiyofyatuliwa, nimejifunza kitu japo mambo ya Ngoswe nawaachia akina Ngoswe.

Niligundua kuwa ukiruhusu wachunaji, sorry wachungaji, mashehena, ashakum, mashehe kuwa wanasiasa, unachganya dini na politiki. Hapa, tatizo ni wawili kudhani wanatumiana wasijue watafyatuana tu katika utapeli wa kuuza dhahabu feki na kulipwa fedha feki.

Huwezi kuwa popo ukakubaliwa na wanyama au ndege. Hatutaki wala hatutavumilia upopo. Lazima tuwapige kipopo.

Nadhani wenzangu walifyatuliwa mkenge pale walipozidiwa kete na matapeli wakidhani wanafyatua kumbe wanafyatuliwa. Sasa kimeumana. Wanafyatuana.

Yao nawaachia. Nirejee kwa mafyatu wangu. Nataka wasome na kuzingatia haya kwa makini. Wahakikishe wanayakariri kama sala ili wasijenigusa pabaya nikwagwijimi kinomi.

Mosi, kuanzia leo, mie ndiyo msemaji pekee wa Chama chetu cha Mafyatu (CccM). Haiwezekani kila fyatu aamke, tena kutoka usingizini au ulevini uwe wa kanywaji au maulaji, kuitisha press conferences na kunifyatua tena hadharani.

Pili, siyo kila jambo lazima liongelewe na yeyote atakaye na anavyotaka. Na si kila ukweli lazima usemwe. Mwingine unauma na kuudhi. Unaambwa mfalme au malkia kauramba halafu unasema eti yuko uchi. Hata kama yu uchi, inakuhusu nini? Mfano, sisi mafyatu tulishakubaliana na baadhi ya mambo kama vile utekanaji, upotezaji, na unyotoaji wa roho za wale wanaotishia ulaji wetu uanofanywa na wasiojulikana na kifo ni kifo ilmradi kisiniguse mimi na familia na marafiki zangu. Pamoja na kujuwa kuwa wasiojulikana wakajulikana ndiyo watekaji, mnaanza kulaumu laumu tu. Sasa tungekuwa tunawanawajua na wasiojulikana wakajulikana, si wangewakamata na kuwanyongelea mbali. Kuweni na subira. Mngoje wasiojulikana wajulikane, kama kweli hawajulikani na hawatajulikana, wakamatwe tukomeshe huu ukatili, unyama, na uzwazwa.

Tatu, hakuna fyatu anayepaswa kupingana na sera zetu. Wewe nani unayejitia kujuajua na kufyatukafyatuka hadi unapingana na sera yetu? Huwezi kuwa ndani na nje kwa wakati mmoja. Kama unataka kuwa nje, toka nje au nitakutoa nje. Pia, ieleweke, hakuna awazaye kuwa ndani akafyatuka kama wale waliioko nje akabaki ndani. Tutamtoa nje huko tulikomuokota kiwa na tongotongo aendelee kuchonga na kufyatua na kufyatuka atakavyo ilimradi achunge wasiojulikana wasimtembelee akaishia kutojulikana alipo kama Mdunde na wengine. Nkikumbushie kwa mara ya mwisho. Fyatu yeyote atakayetaka kukinukisha ili kutisha ulaji na maagizo yangu, atajilaumu mwenyewe pale wasiojulikana watakapomteka, kumpoteza, au kumnyotoa roho.

Nne, ni marufuku kuchanganya dini na politiki kuanzia sasa. Haiwezekani matapeli fulani wakala kuwili kama ndumilakuwili nasi tukawaacha. Sadaka wale wao na maulaji yetu ya kiunene nayo wafaidi. It can’t be. Kama kunisifusifu, kuniimbia mashairi na pambio ni dili, basi nitatumia umoja wa viyanki wetu kufanya kazi hiyo.

Tano, naonya. Yeyote atakayepimana nguvu nami, namfyatua. Ukiwachekea nyani, utakuvuna mabua. Hatuwezi kukupa ulaji wetu ukaugeuza wako na kula na kushiba, kujisahau na kuanza kututapikia na kufichua mambo yetu tusikufystue. Kuanzia sasa, nabatilisha na kupiga marufuku vyeo vya kujipachika. Kila atakayetaka kuhubiria dini mafyatu wangu, lazima awe na shahada ya dini isiyo ya heshima wala kughushi. Hivyo, vyeo vyote vya kujipachika vitachukuliwa kama jinai ya kawaida inayolenga kujitajirisha kwa kuwachuna mafyatu wetu wenye shida mbalimbali. Pia, nisisitize. Wahusika waabudu, kutumikia, na kutukuza miungu yao. Mie sihitaji hayo yote na wajue. Sina subira kama miungu yao. Ukinichengua, tunachenguana na nakufyatua bila kujali kama madai yako ni ya kweli au uongo. Chonde chonde, msiniguse wala kugusa ulaji wangu.

Sita, kuanzia leo, hakuna gea yoyote itakayokubalika kama vile kuniombea maisha marefu, ushindi kwenye uchakachuaji ujao, na mengine mengi kama kunilinganisha na manabii na mitume. It is too much. Mie si nabii wala mtume bali Daktari, Profesa, Jenero, Field Marshal, Papa, Mtakatifu, Mtukufu, Mwenye maono, Mponyaji, Muota ndoto, Mtabiri, Alhaji, Mhashamu, His Excellency, His Eminence, HH etc. Fyatu Mfyatuzi bin Mfyatuaji bin Mfyatukage wa Mfyatulizi mwana wa Mfyatukizi mjukuu wa Fyatuafyatua. Hata kwenye uapisho wangu sitataka kuwaona viumbe hawa wasio na shukrani. Sitaki tena unafiki wa kunipamba kumbe wananiponda.

Mwisho, nachukua fursa hii kuwaomba msamaha mafyatu wangu. Maana, wengi walinitahadharisha kuchanganya dini na politiki nikagoma nisijue ningejutia. Walinionya kuwa wengi walikuja na kunipamba kwa mapambio wakati, nyuma ya pazia, wananiponda na kujiona wajanja kwa kunitumia kupata maulaji yetu ya dezo. Sasa nimewastukia. Lazima niwafyatue kabla hawajanifyatua aka kunigwjiming. Nawahakikishia. Sitafyatuliwa kirahisi tena. Huwezi kunipaka mafuta kwa mgongo wa chupa nisikunyoe bila maji. Hivyo, tusilaumiane wala kuingiliana.

Kwa maoni na ushauri, tuma kwa [email protected]