Prime
“Wanaume tumieni fimbo ndogo, siyo kubwa”

Muktasari:
- Kwa wanandoa, wanajua hii fimbo ni nini na matumizi yake ni yapi ikilinganishwa na fimbo ya kawaida ambayo ni chombo cha kutesa au kuumiza.
Hayo ni maneno ya mama mmoja nchini Kenya aliyekuwa akilalamikia unyanyasaji wa kijinsia nchini humo hasa matumizi ya fimbo kubwa na ngumi baina ya wanandoa.
Alitoa suluhisho ambalo si wengi wangelitegemea kwa kupendekeza fimbo ndogo badala ya kubwa. Kisanii, mama yule alisema, ‘wanaume tumieni ile fimbo ndogo aliyowapea Mungu.”
Kwa wanandoa, wanajua hii fimbo ni nini na matumizi yake ni yapi ikilinganishwa na fimbo ya kawaida ambayo ni chombo cha kutesa au kuumiza.
Tujirejea nchini, kuna unyanyasaji mkubwa wa kijinsia ambapo waathirika wakubwa na wengi ni kinamama japo kuna kinababa ambao pia ni waathirika pamoja na kuwa na fimbo ndogo inayohitajika katika kila ndoa. Kwa sababu tunajadili mambo ya kikubwa, hatuna haja ya kufafanua fimbo ndogo ni nini japo tumefafanua fimbo kubwa. Kama kuna mwanandoa asiyeijua, hii basi, amekosea na kupoteza fedha yake kusoma makala haya. Hayo tunawaachia.
Sasa tuje kwenye pendekezo la kutumia fimbo ndogo. Tutauliza swali la kichokozi. Hili ni kwa wanandoa tu ijapokuwa hata wasio wanandoa huiiba na kujikuta katika tutakachouliza katika swali hili.
Je, kati ya vyakula, ni chakula gani ambacho walaji hawachoki kula? Sambamba na hili, ukimchapa mtu kwa fimbo ndogo, yupo tayari upige hadi ‘uue’ kama mambo unayaweza lakini achapwe tu.
Tunadhani tunaelewana. Pia, tuvumiliane. Haya mambo japo tunayaongea kiutu uzima, lazima yasemwe.
Sasa jiulize. Kama kila mwanaume kajaaliwa fimbo ndogo, kwanini asiitumie wakati wanaopigwa kwayo wanaitaka, hawalalamiki, kuchoka, wala kuchukia kupigwa kwayo wakati wako tayari kuchapwa hadi ‘wauawe?”
Hamkumsikia mchungaji fulani msanii akisema kuwa mchunge watoto wasisikie ‘niue, niue tu.” Je, mtafanya nini? Huyu mtaalamu wa mambo haya anapendekeza mnapoanza ‘ugomvi’, fungulieni radio au runinga zenu kwa sauti ya juu ili watoto wasianze kuuliza maswali yasiyo na majibu. Tunadhani tunaelewana mpaka hapa.
Turejee kwenye fimbo ndogo. Kwanza, haiumizi japo yaweza kufanya anayepigwa kulalamika. Pili, haikatiki wala haihitaji kuchuma kwenye mti au porini.
Tatu, inabebeka kirahi kiasi cha mwenye kuwa nayo kuwa nayo kila mahali alipo. Hivyo, hata kuitumia si vigumu.
Ila chungeni. Haifai kupigia kila mtu bali mmoja au idadi ya wapigwaji kwa mujibu wa dini na mila zenu.
Nne, tofauti na fimbo kubwa, fimbo ndogo haina madhara yoyote ya kiafya iwe kiakili au kimwili wala haihusishwi na ukatili wa kijinsia, unyanyasaji labda ikitumiwa vibaya kwa kuvuka mipaka na kugeuka cha wote.
Isitoshe, fimbo hii ni dawa ya malazi mengi kama vile kukosa usingizi, mawazo, uchovu, unyong’onyevu, upweke, njaa ya chakula cha usiku,na mengine mengi kama hayo.
Tano, kwa wanaojua matibabu ya viboko au acupunture, wanajua namna fimbo inavyoweza kutumika kutibu magonjwa mbalimbali.
Tofauti na tiba viboko, fimbo ndogo, tusisitize siyo kwa kila mgonjwa au wale ambao hawajaingia kwenye ndoa japo wapo wanaoiba tiba hii na kuishia kusababishiana madhara badala ya matibabu.
Sita, japo fimbo hii ni tiba, haihitaji fedha kuinunua wala kutumia mara moja na kutupa. Ukishaipata umeipata, vinginevyo mwenye kuitumia augue au kufariki.
Ipo saa 24 kwa ajili ya mgonjwa wake na tabibu wake. Hivyo, ukiondoa hayo juu, tiba ya ‘acupunture’ ipo muda wote na mahitaji ni wakati wote.
Saba, japo kuna madaktari uchwara wanaosema isitumike kila siku, kwa uzoefu wetu, haina madhara yoyote ikitumika kila siku. Ni sawa na lishe au tiba yoyote ya kuongeza afya.
Watu wazima tena wapendanao hawapigani kwa fimbo kubwa wakati ndogo ipo na inakubalika. Fimbo kubwa wamepangiwa wanyama wanaoswagwa kwenda malishoni au shambani tena kwa kulazimishwa siyo kutaka kama ilivyo fimbo ndogo kwa wanandoa.
Kwa watu wa pwani kuna msemo maarufu kuwa mke hapigwi kwa fimbo (kubwa) ila kwa upande wa khanga. Hapa, tunadhani wanamaanisha fimbo kubwa na siyo ndogo.
Japo si mwarobaini bali zaidi, hayo ndiyo manufaa na matumizi ya fimbo ndogo. Tunatoa wito kwa wanandoa wote kuanza kutumia fimbo ndogo tu na kuachana na fimbo kubwa inayosababisha mateso na ukatili kwa kinamama walio kwenye ndoa. Mwisho, kama unaweza kuua kwa asali, kwanini utumie sumu?