Wawili wafariki, 12 wajeruhiwa ajali ya basi na lori Iringa
Iringa. Watu wawili wamefariki dunia na wengine 12 kujeruhiwa baada ya basi la kampuni ya Classic lililokuwa likitoka Zimbabwe kuelekea Dar es Salaam kugongana na lori eneo la Mseke, Kata ya Kitwiru, mkoani Iringa.
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa, Dk Alfredy Mwakalebela, amesema ajali hiyo ilitokea leo Jumatatu, Mei 11, 2026, saa 11 alfajiri, na majeruhi 13 wamefikishwa hospitalini hapo kwa matibabu.
Amesema kati ya majeruhi hao, 10 wamepata majeraha ya kawaida huku watatu wakiwa katika hali mbaya, akiwemo mjamzito na mwanaume mmoja. Aidha, maiti mbili zilizopokelewa hospitalini hapo ni za madereva wa lori na basi hilo.
Kwa mujibu wa Dk Mwakalebela, majeruhi wengi ni raia wa kigeni, ambapo wanne ni kutoka Zambia, wanane Zimbabwe na mmoja ni Mtanzania.
Mfanyakazi wa basi hilo, Abdallah Abdi, amesema dereva wa lori alilivaa basi hilo na kulazimika kulikwepa kwa kuingia porini. Amesema basi hilo lilikuwa limebeba abiria 30 waliokuwa wakitoka Zimbabwe kuelekea Dar es Salaam.
Endelea kufuatilia Mwananchi….