Washtakiwa wanaodaiwa kuchana noti kuhojiwa polisi Dar
Muktasari:
- Mahakama ya hakimu mkazi Kisutu imeridhia ombi la upande wa mashtaka kutaka washtakiwa 13 wakiwemo watumishi nane wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuhojiwa kituo cha polisi kati jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kukamilisha upelelezi wa kesi hiyo.
Dar es Salaam. Mahakama ya hakimu mkazi Kisutu imeridhia ombi la upande wa mashtaka kutaka washtakiwa 13 wakiwemo watumishi nane wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuhojiwa kituo cha polisi kati jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kukamilisha upelelezi wa kesi hiyo.
Washtakiwa hao ni Mariagoretha Kuzugala, Henry Mbowe, Asha Sekiboko, Cecilia Mpande, Agripina Komba, Zubeda Mjewa, Khadija Kassunsumo na Mwanakheir Omary.
Wengine ambao si watumishi wa BoT ni, Alistides Genand, Shukuru Mchegage, Musa Chengula, Zaituni Chihipo na Respicius Ishengoma.
Wote wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi yenye mashtaka sita likiwemo kuharibu noti za Sh4.6 milioni kwa kuzichana na kuisababishia BoT hasara ya Sh4.6 bilioni.
Ombi hilo limewasilishwa mahakamani hapo na wakili wa Serikali, Ester Martin mbele ya hakimu mkazi mfawidhi mahakama hiyo, Godfrey Isaya.
Martin amesema wanaomba kibali cha siku moja kwa ajili ya washtakiwa hao kuhojiwa kituoni hapo kwa ajili ya kukamilisha upelelezi.
Ombi hilo lilikubaliwa na hakimu huyo na kwamba baada ya mahojiano hayo washtakiwa hao wanatakiwa kurudishwa gerezani kwa sababu mashtaka yanayowakabili likiwemo la kutakatisha fedha halina dhamana kwa mujibu wa sheria.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Februari 22, 2021 itakapotajwa.
Katika kesi ya msingi wanadaiwa kati ya Januari 2017 hadi Septemba 30, 2019 jijini Dar es Salaam watumishi hao wa BoT kwa kuvunja majukumu yao ya kazi waliwezesha utendekaji wa kosa la kuongoza genge la uhalifu.
Shtaka jingine katika tarehe hizo jijini Dar es Salaam bila ya kuwa na kibali na kutokuwa wazalendo waliharibu noti za Sh4.6 milioni.