Vurugu zazuka uchaguzi Chadema Kanda ya Nyasa

Wafuasi wa Chadema Kanda ya Nyasa wakiwa katika purukushani mlangoni katika ukumbi wa Kanisa Katoliki Parokia ya Bikra Maria wa Neema katika mji wa Makambako. Picha na Saddam Sadick
Njombe. Ikiwa inaelekea uchaguzi wa kuwapata Mwenyekiti, Makamu na Mweka Hazina wa Chadema Kanda ya Nyasa, vurugu zimeibuka na kusababisha mvutano baina ya makada wa chama hicho.
Hata hivyo, haikufahamika haraka chanzo cha vurugu hizo, ambapo wakati wajumbe wa mkutano mkuu wakiendelea kuingia ukumbini, ghafla baadhi ya waliokuwa wametangulia walirejea tena getini wakitishia kususia uchaguzi.
Waandishi wa habari hawajaruhusiwa kuingia ndani ya geti wala ukumbini wakielekezwa eneo maalumu la kukaa kusubiri wagombea watakapoingia ndani ndio wataruhusiwa kwa dakika kadhaa.
Walinzi wa chama hicho walikuwa makini kuingilia kati vurugu hizo, huku baadhi wakielekezwa kuwaondoa wanaotishia kususia uchaguzi huo.
Licha ya kutokea vurugu hizo, amani imerejea hadi sasa wajumbe wanaendelea kuhakikiwa kwa ajili ya kuingia ukumbini kusubiri hatua ya uchaguzi kuwapata viongozi wa Kanda.