Tarura yataja mtandao wa barabara utakaojengwa

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), Victor Seff akizungumzia utekelezaji wa majukumu na mwelekeo wa utekelezaji wa majukumu ya Tarura kwa mwaka wa fedha 2023/24. Picha na Sharon Sauwa
Muktasari:
- Wakati msimu wa mvua ukikaribia kuanza nchini, Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (Tarura) umeelezea mtandao wa barabara utakaotejengwa katika mwaka wa fedha 2023/24.
Dodoma. Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (Tarura), umetengewa Sh858.51 bilioni kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa barabara za wilayani katika mwaka wa fedha 2023/24.
Hayo yamesemwa leo Alhamis Agosti 24, 2023 na Mtendaji Mkuu wa Tarura, Victor Seff, wakati akielezea utekelezaji wa majukumu na mwelekeo wa utekelezaji wa majukumu katika mwaka wa fedha 2023/24.
“Katika mwaka wa fedha 2023/24, jumla ya barabara zenye kilometa 21,057.06 zitafanyiwa matengenezo, kilometa 427 zitajengwa kwa kiwango cha lami, kilometa 8,775.62 zitajengwa kwa kiwango cha changarawe, huku madaraja na makalavati 855 pamoja na mifereji ya mvua kilometa 70, kujengwa,” amesema.
Seff amesema wamekwishatangaza kazi za ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara zaidi ya asilimia 60 ya mpango wa mwaka 2023/24 ambapo baadhi ya kazi utekelezaji umeanza.
Akizungumzia kuhusu matumizi ya teknolojia mbadala, Seff amesema miongoni mwa vipaumbele vya Tarura ni kutumia malighafi zinazopatikana maeneo ya kazi ili kupata ufanisi wa gharama za ujenzi.
Amesema hadi Machi mwaka 2023, Tarura imejenga madaraja 163 ya mawe yenye thamani ya Sh8.7 bilioni ambapo gharama imepungua kwa zaidi ya asilimia 50.
Idadai ya katika na mabano na mikoa ilikojengwa ni pamoja na Kigoma (92), Singida (24), Tabora (5), Kilimanjaro (10), Mbeya (2), Arusha (6), Morogoro (2), Rukwa (3), Pwani (1), Ruvuma (3) na Iringa (15).