Mwili wafukuliwa baada ya kukaa kaburini siku 53

Mwili wa Yunami Massawe (34) mkazi wa kijiji cha Nkwansira Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro ukitolewa kwenye kaburi baada ya kukaa kwa siku 53. Picha na Dionis Nyato
Muktasari:
Mwili wa Yunami Massawe (34) ambaye alifariki dunia Februari 27 mwaka huu, umefukuliwa baada ya kukaa kaburini kwa siku 53 ili kufanyiwa uchunguzi wa kitabibu (postmortem).
Hai. Mwili wa Yunami Massawe (34) ambaye alifariki dunia Februari 27 mwaka huu, umefukuliwa baada ya kukaa kaburini kwa siku 53 ili kufanyiwa uchunguzi wa kitabibu (postmortem).
Yunami ambaye alidaiwa kuwa alipata ajali ya pikipiki eneo la Shangarai mkoani Arusha alizikwa Machi 4 mwaka huu katika Kijiji cha Nkwansira Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro ambapo baadaye kuliibuka utata wa kifo chake na familia yake waliomba kibali cha kuufukua mwili huo ili ufanyiwe uchunguzi.
Machi mwaka huu familia ya kijana huyo iliomba kufungua shauri kufukua mwili ili ufanyike uchunguzi wa kitabibu baada ya kuibuka utata wa chanzo cha kifo cha kijana huyo kutokana na madai kuwa aliuawa kwa kipigo cha mke wake na baba mkwe.
Mpaka sasa mke wa marehemu, Sarah Meshack Mollel pamoja na baba mkwe wake, Meshack Mollel wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani Arusha baada ya familia ya marehemu kuwafungulia kesi namba USR/IR/619/2022.
Akizungumza baada ya kufukuliwa kwa mwili huo leo Jumatano Aprili 27, 2022, kaka wa marehemu, Elimmwaria Massawe amesema “Sisi kama familia tunaishukuru sana Serikali kupitia Ofisi za Mashtaka Mkoa wa Arusha na Kilimanjaro walivyopokea maombi yetu ya mwili wa ndugu yetu ufukuliwe upya kutokana na utata uliojitokeza kwenye kifo cha mdogo wetu,"
"Kama familia tunashukuru kwa kilichofanyika leo tunaimani Serikali itasimamia hili na haki ya ndugu yetu itapatikana,"amesema Massawe.
Hata hivyo baada ya mwili huo kufukuliwa ulizikwa tena baada ya kuchukuliwa vipimo vya kitabibu ili kubaini hasa chanzo cha kifo cha kijana huyo.