Mwapachu awashukia watendaji wa EAC nchini

Katibu Mkuu Mstaafu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Juma Mwapachu akizungumza kwenye kikao cha utoaji ripoti iliyofanywa na taasisi ya TWAWEZA kuhusiana na uungaji mkono wa wananchi kwa Jumuiya hiyo uliofanyika jijini Dar es Salaam jana. Kutoka kushoto ni Mtafiti wa TWAWEZA, Elvis Mushi na Mkurugenzi Mkuu , Rakesh Rajan . Picha na Rafael Lubava
Muktasari:
Ni kuhusu kusuasua kwa utekelezaji wa baadhi ya makubaliano na wanachama wengine.
Dar es Salaam. Aliyekuwa katibu mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Balozi Bakari Mwapachu amesema viongozi wa Tanzania wamekuwa nyuma katika utekelezaji wa baadhi ya makubaliano muhimu ya jumuiya hiyo.
Baadhi ya masuala hayo ni pamoja na utekelzaji wa soko la pamoja, ujenzi wa miundombinu na hati ya kusafiria ya pamoja, hali inayofanya nchi nyingine wanachama kuanzisha mikakati yao ya kuharakisha mchakato huo.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa utafiti wa Awamu ya 23 ya Sauti za Wananchi uliofanywa na taasisi isiyo ya kiserikali ya Twaweza kwa ushirika wa taasisi ya Society for International Development (SID), Mwapachu alisema Watanzania wengi wanataka mambo mazuri yaliyopo kwenye makubaliaono ya EAC, lakini viongozi ndiyo wanaochochea ucheleweshaji wake.
Alisema hata hatua ya Kenya, Uganda na Rwanda kuungana kuharakisha mchakato wa ujenzi wa miundombinu na taratibu nyingine, huenda ilichochewa na kusuasua huko na kwamba nchi hizo hazikuvunja utaratibu wowote wa kisheria.
“Ushirikiano wa hiari ni dhana ya kisheria siyo dhana potofu kama wengine wanavyodai na mkataba wa kuanzisha EAC unaruhusu jambo hilo,” alisema Balozi huyo.
Hata hivyo, alibainisha kuwa mwaka 2008 baadhi ya wataalamu walishauri kuwa ushirikiano wa hiari ulitakiwa kufanywa kwa tahadhari kwa kuwa EAC ina nchi chache zinazoweza kulegeza utengamano.
Katika utafiti uliofanywa kwa njia ya simu za mkononi kati ya Agosti 13 hadi 22 mwaka huu katika kaya 1,408 za Tanzania Bara watu nane kati ya 10 wanaamini kuwa Tanzania inapaswa kubaki kuwa mwanachama wa jumuiya hiyo.