Mama aliyejifungua sakafuni augua, alazwa

Muktasari:
- Wakati mwili wa kichanga uliotelekezwa katika Hospitali ya Wilaya ya Hai, Kilimanjaro kwa siku tano ukizikwa, mama wa kichanga hicho ameugua ghafla na kurudishwa hospitalini hapo.
Hai. Wakati mwili wa kichanga uliotelekezwa katika Hospitali ya Wilaya ya Hai, Kilimanjaro kwa siku tano ukizikwa, mama wa kichanga hicho ameugua ghafla na kurudishwa hospitalini hapo.
Akizungumza na Mwananchi akiwa hospitalini hapo, Happiness Massawe alisema baada ya kupata ushauri kutoka kwa viongozi wa dini, familia iliamua kuchukua mwili wa kichanga na kwenda kuzika katika makaburi ya kanisa yaliyopo Kimaroroni Kata ya Rundugai.
Alisema baada ya maziko alirejea nyumbani ambako uongozi wa hospitali ulimtembelea na kukuta hali yake ni mbaya, ndipo ukamchukua na kumpeleka hospitali ambapo anaendelea na matibabu
“Kinachonisumbua ni kichwa, mgongo na tumbo na kifua kinabana ila naona napata huduma vizuri na hali yangu inaenda ikiimarika,” alisema Happiness.
Mganga mfawidhi wa hospitali hiyo, Dk Itikija Msuya alisema kamati iliyoundwa kuchunguza sakata na mama huyo kujifungulia sakafuni huku watoa huduma wakimwangalia, haijaleta majibu lakini kichanga kimechukuliwa na kuzikwa.
Happiness (39), aligoma kuchukua mwili wa mwanaye kwa takriban wiki moja katika hospitali ya wilaya ya Hai, kwa madai kifo chake kimetokana na uzembe wa wauguzi.