Bashe: Sh200 bilioni kutumika kutoa ruzuku ya mbolea msimu huu

Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe akitoa maelezo kwa Rais Samia. Picha na Ikulu
Muktasari:
- Waziri wa Kilimo Hussein Bashe amesema zaidi ya Sh200 bilioni zinatarajiwa kutumika katika kutoa ruzuku ya mbolea kwa wakulima katika msimu huu wa kilimo.
Dar es Salaam. Waziri wa Kilimo Hussein Bashe amesema zaidi ya Sh200 bilioni zinatarajiwa kutumika katika kutoa ruzuku ya mbolea kwa wakulima katika msimu huu wa kilimo.
Kuwekwa kwa fedha hizo kutafanya matumizi ya mbolea katika msimu huu kufikia tani 650,000
Ameyasema hayo leo katika kilele cha maadhimisho ya siku ya wakulima Nanenane kilichofanyika katika uwanja wa John Mwakangale jijini Mbeya.
"Tunatarajia matumizi ya mbolea yatafika tani 650,000, katika msimu huu, pia tunashukuru kwa kutupatia Sh100 bilioni kwa ajili ya kufufua kampuni ya mbolea Tanzania (TNFC) ambayo sasa imeshaagiza mbolea na imeanza kusambaza katika maeneo mbalimbali nchini," amesema Bashe.
Bashe amesema pia kwa sababu kufikisha mbolea katika ngazi ya kata ni kazi, wameongeza vyama vya ushirika ili viwe wasambazaji wa mbolea hiyo jambo ambalo litaondoa tatizo la wakulima kupata mbolea.
Akitaja bei mpya ya baadhi ya mbolea baada ya bei za ruzuku Bashe amesema Mbolea ya SA itakuwa kati ya Sh45000 hadi Sh52000 badala ya Sh85000
Huku NPk zote zikiwa Sh70, 000 hadi Sh85 000. Mbolea ya viwanda vya ndani zitakuwa kati ya Sh68, 000 hadi Sh750, 000.