Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

‘Mtanzania’ ashinda udiwani London

Raia wa Uingereza mwenye asili ya Tanzania, Linda Lusingu

Muktasari:

Raia wa Uingereza mwenye asili ya Tanzania, Linda Lusingu ameshinda udiwani kata ya East Barnet, iliyoko mji mkuu wa London kwa kuwashinda wagombea wenzake 10 katika uchaguzi uliofanyika Mei 5, mwaka huu.

Dar es Salaam. Raia wa Uingereza mwenye asili ya Tanzania, Linda Lusingu ameshinda udiwani kata ya East Barnet, iliyoko mji mkuu wa London kwa kuwashinda wagombea wenzake 10 katika uchaguzi uliofanyika Mei 5, mwaka huu.

Lusingu ambaye ni mtaalamu wa sheria za familia na watoto, ameshinda uchaguzi huo kupitia chama cha Labour na ushindi wake amechangia chama hicho kuwa na madiwani wengi katika Halmashauri ya Barnet iliyokuwa ikiongozwa na chama cha Conservative kwa miaka mingi.

Akizungumza na kituo cha televisheni cha Azam na baadaye Mwananchi, Lisungu ambaye ni mwenyeji wa Same, Kilimanjaro, alisema amekuwa mwanachama wa Labour kwa miaka 13 na kwake imekuwa safari ndefu hadi kushinda nafasi hiyo.

“Haikuwa rahisi kufikia hapa, hasa ukichukulia kuwa natoka kwenye jamii za watu weusi wachache ambao hawana uwakilishi, sikuzaliwa huku na siyo mtu mweupe, kwa hiyo kuna ubaguzi mwingi.

“Nilikwenda Uingereza nikiwa na umri wa miaka 15 na nimeishi huku kwa miaka 23. Niliingia kwenye mambo ya siasa karibu miaka 13 iliyopita baada ya kumaliza masomo ya chuo na nikapata nafasi ya kufanya kazi kwa mbunge sehemu niliyokuwa nakaa na huo ndio ukawa mwanzo wa safari hii,” alisema Lusingu.

Alisema kwa kipindi hicho alifanya naye kazi na kuona anavyofanya na kusaidia watu kwenye jamii, kama yeye alivyofika huko akiwa na mambo mengi yaliyohitaji msaada wake ikiwemo viza, nyumba na mambo mengine ambayo kama wageni wangehitaji.

“Aliponipa hiyo nafasi nikaona ni nafasi nzuri na nikaendelea kuwa kwenye chama na ilipokuja hiyo nafasi nikaamua kuwania,” alisema.

Alieleza kuwa kama wanachama wa Labour walifanya kazi sana kwa kuongea na wakazi wa eneo hilo kuhusu shida zao, hasa ugumu wa maisha, gharama za kuishi na kutofurahia mambo yaliyofanywa na Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Borris Johnson kama marufuku ya kufungia watu (lockdown) wakati wa Uviko-19.

“Watu walipoteza ndugu zao kipindi hicho ingawa yeye alikuwa akifanya sherehe, na sheria alizoziweka alikuwa hazifuati, hicho kiliumiza watu wengi na hiyo ilitusaidia kidogo kushinda.

“Lakini la muhimu ni kwamba tulifanya kazi na kuongea nao, lakini tuliwapa ilani ambayo wao waliamua kutuunga mkono na ndiyo maana tumeshinda.”

Licha ya Serikali ya Waziri Mkuu wa nchi hiyo kufanya vibaya kwenye uchaguzi huo, anaamini ushindi wa Labour umetokana na sera na ilani aliyosema ilileta matumaini kwa wananchi waliokata tamaa. Alisema alikwenda Uingereza wakati baba yake akisoma huko na yeye kusomea huko. Kwa sasa baba yake amesharudi Tanzania.