Awapa ujauzito wanawake watano kwa mpigo

Muktasari:
- Awafanyia sherehe kwa wakati mmoja, akiacha gumzo kwa jamii
Taarifa mpya
Marekani. Lizzyash Ashliegh, ambaye ni chanzo cha kusambaa video kwenye mitandao ya kijamii akieleza yeye na wenzake wanne walipewa ujauzito kwa mpigo na mwanamuziki wa Marekani, Zeddy Will, ameibuka kukanusha.
Kupitia mtandao wa Tiktok, Lizzyash amesema hana ujauzito, bali kilichotokea ni kwamba walikuwa wakiandaa video ya muziki.
Lizzyash akisema hayo, taarifa zake za awali kuhusu yeye na wenzake wanne kuandaliwa sherehe kabla ya mtoto kuzaliwa (Baby Shower) zimeendelea kuonekana kwenye tovuti mbalimbali, zikiwamo Daily Mail, India Today, New York Post, The Economic Times na Complex.
“Usiamini kila kitu unachokiona kwenye mtandao. Hii imesambaa sana! Makala za runinga za habari zinazochapisha uandishi wa habari feki, mimi si mjamzito, hii ilikuwa kwa ajili ya video ya muziki ambayo sikuwa na ruhusa ya kusema hivyo,” ameandika Lizzyash kwenye mtandao wa Instagram.
Taarifa za awali.
Katika hali ya kushangaza, mwanamuziki nchini Marekani, Zeddy Will amewafanyia sherehe wanawake watano aliowapa ujauzito kwa mpigo.
Sherehe hiyo kabla ya mtoto kuzaliwa (Baby Shower) imegeuka gumzo kwenye mitandao ya kijamii, wengi wakihoji ni njia gani ameitumia kuwafanya wanawake hao kuelewana na kukubali kushiriki sherehe hiyo ya pamoja.
Kwa mujibu wa tovuti ya Daily Mail, tukio hilo lilionekana kwa mara ya kwanza kupita mtandao wa kijamii wa Tiktok ambako picha ya mjongeo (video) ilichapishwa na mmoja wa wanawake hao.
Lizzy Ashleigh, ndiye alichapisha video hiyo huku akiweka wazi juu ya sherehe hiyo iliyofanyika Januari 14, 2024.
Mwaliko wa sherehe hiyo ulikuwa umeambatanishwa na maneno yasemayo, "Welcome little Zeddy Wills 1-5."
Wanawake wengine waliopewa ujauzito na mwanamuziki huyo mwenye umri wa miaka 22 ni Bonnie B, Jylene Vila, Kay Marie, na Iyanla Kalifa Galletti.
Akizungumzia tukio hilo kupitia chapisho lake, Ashleigh aliambatanisha ujumbe unaosema “Nadhani sasa ni wake wenza.”
Picha hizo za sherehe ya kujiandaa kuwapokea watoto zilikuwa zimepambwa na nyuso za tabasamu, huku video za wanawake hao zilionyesha wakifurahi na kucheza.
Zeddy, baba mtarajiwa wa watoto hao watano alionekana katika moja ya picha akiwa katikati ya wanawake hao, Ashleigh alimtambulisha.
Mwanamke huyo amesema wote kwa pamoja wamekubali kuelewana kwa faida ya watoto wao ambao watakuwa ndani ya familia kubwa.
Imeandikwa na Mwandishi Wetu kwa msaada wa mtandao.