Aunt Ezekiel sasa ni Rahma afunga ndoa na Kusah
Muktasari:
- Baada ya kubadili dini, Aunt Ezekiel sasa anaitwa Rahma, jina ambalo alilitumia kwenye ndoa yake ya kwanza mwaka 2012 alipooolewa na mfanyabiashara, Sunday Dimonte.
Dar es Salaam. Nyota wa filamu za Kibongo, Aunty Ezekiel, amebadili dini kutoka Ukristo na kuwa Muislam baada ya kuolewa na msanii wa Bongofleva, Kusah.
Baada ya kubadili dini, Aunt Ezekiel sasa anaitwa Rahma, jina ambalo alilitumia kwenye ndoa yake ya kwanza mwaka 2012 alipooolewa na mfanyabiashara, Sunday Dimonte.
Kwa mujibu wa Kusah, amemuona Aunt Ezekiel miezi kadhaa iliyopita kwa kufuata taratibu zote za dini ya Kiislamu, ambapo ndoa hiyo ilikuwa kimya kimya bila ya kufanya sherehe.
"Kwa sasa Aunt Ezekiel anaitwa Rahma, amebadili dini na tukafunga ndoa kimya kimya, tulifuata taratibu zote za dini ya Kiislamu, sasa rasmi ni mke wangu ambaye amenizalia watoto wawili," amesema Kusah.
Kusah alitoa sababu ya kufunga ndoa kimya kimya, bila ya sherehe kubwa kama baadhi ya wasanii wengine walivyofanya ambapo amesema ni kutokana na kuona hatua kubwa ya kufunga ndoa ilitimia hivyo sherehe haikuwa na ulazima sana.
"Hapana, sikutaka kufanya sherehe kubwa, sababu lile ambalo tumekusudia kulifanya la kufunga ndoa ndio lilikuwa muhimu sana kuliko sherehe, hivyo hakukuwa na ulazima sana kufanya sherehe," amesema Kusah.
Kwa upande wa Aunt Ezekiel, Mwananchi ilimuuliza sababu ya kurudia jina ambalo alishawahi kutumia kwenye ndoa yake ya kwanza ambapo amesema:
"Sikuona kuhangaika kutafuta jina lingine la Kiislamu wakati tayari nilishakuwa na jina hapo awali pindi nilipoolewa, na pia jina la Rahma nalipenda sana, niseme tu sikuwa na wazo kabisa na ndoa tena, lakini nikawa tayari sababu ya kuona niliyekuwa naye ni sehemu sahihi kwangu, sikuweza kupinga pale aliponiambia anataka tufunge ndoa, jamani Kusah ni mwanaume haswa yaani ni baba bora na sio bora baba."
Hii ni ndoa ya pili kwa Aunt Ezekiel kufunga kimyaa kimya, ya kwanza ilikuwa mwaka 2012 nchini Dubai alipofunga na mfanyabiashara, Sunday Dimonte.
Mwaka 2014, ndoa hiyo ilivunjika na Aunt Ezekiel kurudi kwenye dini yake ya Ukristo.
Kwa upande wa Kusah na Aunt Ezekiel, toka waanzishe mahusiano ya kimapenzi, hadi sasa wana miaka mitano na wamefanikiwa kupata watoto wawili wa kiume na wa kike.
Wawili hao kabla ya kuanzisha mahusiano hayo, tayari walishapata watoto na mahusiano yao mengine, ambapo Kusah alipata mtoto na msanii wa Bongofleva, Ruby, huku Aunt Ezekiel akipata mtoto na mcheza shoo wa msanii wa Bongofleva, Diamond aitwaye Mose Iyobo.