Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

ACT yaeleza sababu Wawakilishi wake kutohudhuria uzinduzi wa Baraza

Mnadhimu wa Chama Cha ACT Wazalendo katika Baraza la Wawakilishi, Profesa Omar Fakih akizungumza na waandishi wa Habari makao makuu ya ofisi za chama hicho Vuga,  Unguja Zanzibar. Picha na Jesse Mikofu

Muktasari:

  • Baraza la 11 la Wawakilishi lilizinduliwa jana Novemba 10, 2025 na Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Mwinyi kama inavyoeleza Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984.

Unguja. Chama cha ACT Wazalendo kimeeleza sababu za wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wanaotokana na chama hicho kutohudhuria uzinduzi wa baraza hilo, ikiwa ni pamoja na kutoridhishwa na yaliyotokea kwenye uchaguzi.

Baraza la 11 la Wawakilishi lilizinduliwa jana Novemba 10, 2025 na Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Mwinyi kama inavyoeleza Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumanne Novemba 11, 2025, mjini Unguja, Mnadhimu wa chama hicho katika Baraza la Wawakilishi, Profesa Omar Fakih amesema walikubaliana kutoshiriki uzinduzi huo kutokana na kutokubaliana yaliyotokea katika uchaguzi.

“Tulitafakari tukio la uzinduzi wa baraza, kwa sababu hatukubaliani na ushindi wake, tukaona kuhudhuria tukio hilo ni kuwadhihaki na kuwacheza shere na kuwatonesha vidonda Wazanzibari,” amesema Profesa Omar.

Chama hicho kina jumla ya wawakilishi 14 ndani ya Baraza hilo, 10 kati ya hao wamechaguliwa majimboni na wanne wanatokana na viti maalumu.

Hata hivyo, Profesa Omar amesema hatua hiyo haiwazuii kuhudhuria vikao vingine vya baraza kwa sababu wao wamechaguliwa na wananchi na wanakwenda kuwawakilisha wananchi ndani ya chombo hicho mpaka itakapokuwa imeamuliwa vinginevyo na chama.

“Tukiwa katika Baraza la Wawakilishi tutatumia ubora wa hoja, kuliko wingi wa hoja katika kutetea haki za Zanzibar na watu wake pamoja na wageni waishio visiwani hapa.”

Amesema wawakilishi wanaotokana na ACT na ambao tayari wamekula kiapo cha kuwatumikia Wazanzibari na Zanzibar, bila kujali uchache wao katika Baraza la Wawakilishi, wataifanya kazi hiyo kwa uaminifu.

“Tunaamini tuna uwezo wa kuhakikisha tunajenga na kusimamia hoja za kuwatetea Wazanzibari juu madhila mbalimbali wanayopitia, tunaazimia kuisimamia Serikali juu masuala mbalimbali yakiwemo ya uchumi wao ili wawe na maisha nafuu na ya staha,” amesema.

Akizungumza kuhusu kuingia kwenye Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), mjumbe huyo wa kamati ya uongozi kitaifa, amesema kwa sasa sio kipaumbele chao isipokuwa wanaangalia masilahi ya wananchi na yale yaliyoharibika ili kupigania haki.

Kauli ya kuwa ndani ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa kuwa sio kipaumbele, pia, ilitolewa na Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Othman Masoud katika mikutano yake ya kuwashukuru wananchi kukipigia chama hicho kisiwani Pemba.

Othman ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar anayemaliza muda wake, alisema kipaumbele chao kwanza ni kusimamia haki za wananchi.

Mpaka sasa, hakuna kauli rasmi iliyotolewa na chama hicho iwapo wanaigia tena katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa au vinginevyo.

Licha ya Katiba ya Zanzibar kumpa nguvu Rais aliyechaguliwa kuteua Makamu wa Kwanza na wa Pili ndani ya siku saba tangu alipoapishwa, lakini Katiba hiyohiyo inatoa siku 90 kwa chama ambacho kimekidhi sifa za kuingia ndani ya SUK kufanya uamuzi.

Jana, wakati akizindua Baraza hilo, Dk Mwinyi alisema yupo tayari kutekeleza maridhiano na kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), licha ya ACT kudai hilo ni takwa la kikatiba wala sio hiari ya mtu.

Naye Katibu wa Itikadi, Habari na Mawasiliano wa chama hicho, Salim Bimani, kama walivyosema wengine, alisema msimamo wa chama utaendelea kutolewa kadri watakavyokuwa wanakubaliana.