Simba kumrudisha Barbara Gonzalez, kuongoza bodi

Muktasari:

  • Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Klabu ya Simba, Salim Abdallah 'Try Again' na mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi, Rashid Shangazi wamegomea uamuzi wa Rais wa heshima wa klabu hiyo akiwataka waandike barua ya kujiuzulu.

KUNA kitu kinaendelea ndani ya Simba usiku huu. Huenda kufikia kesho yakatokea mabadiliko makubwa kwenye uongozi wa juu. 

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Klabu ya Simba, Salim Abdallah 'Try Again' na mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi, Rashid Shangazi wamegomea uamuzi wa Rais wa heshima wa klabu hiyo akiwataka waandike barua ya kujiuzulu.

Rais wa heshima wa Simba, Mohammed Dewj ‘MO’inaelezwa kuwa amewapigia wajumbe wa upande wake akiwataka waandike barua za kujiuzulu kwa lengo la kuunda safu mpya ya uongozi wawili hao wanadaiwa kugomea agizo hilo hadi sasa.

Kwa mujibu wa chanzo cha kuaminika kutoka ndani ya Simba kimeliambia Mwananchi kuwa ni viongozi hao wawili pekee wamegomea wito wa kiongozi wao ambaye ndiye aliyewateua huku wakihoji mambo kadhaa.

“Hadi sasa Try Again na Shangazi hawajaandika barua lakini wengine wote tayari kama mambo yataenda sawa kesho au keshokutwa Barbara Gonzalez atatangazwa  kuwa Mwenyekiti na CEO anatafutwa,” Mwanaspoti limedokezwa.

“Simu hizo amepiga kwa wajumbe wa upande wake pekee kwani ndio ambao anauwezo wa kufanya uamuzi huku kwa upande wa klabu viongozi waliopitishwa na wanachama kwenye mkutano mkuu wanaendelea na majukumu yao kama kawaida.” Kimesema chanzo hicho.