Gyokeres kuifuata Arsenal Asia
London, England. Viktor Gyokeres anatarajiwa kusafiri haraka kuelekea barani Asia kujiunga na kambi ya maandalizi ya msimu mpya ya Arsenal ambayo itakuwa katika nchi za Singapore na Hong Kong baada ya juzi timu hiyo kufikia makubaliano na Sporting Lisbon kwa ajili ya uhamisho wa nyota huyo mwenye umri wa miaka 27.
Kama ilivyo kwa mchezaji mwingine ambaye Arsenal imemnasa katika dirisha hili la usajili la majira ya kiangazi ambaye ni beki Cristhian Mosquera, Gyokeres atafanyiwa vipimo vya afya hukohuko Singapore ingawa meneja wa Arsenal, Mikel Arteta inaripotiwa alipanga jambo hilo lifanyike London, England.
Baada ya mjadala wa muda mrefu uliohusu malipo ya fedha za ziada katika uhamisho wa mshambuliaji huyo raia wa Sweden, Sporting Lisbon juzi iliridhia nyota wake huyo kuitumikia Arsenal kuanzia msimu ujao.
Uhamisho huo ulikuwa ukamilike tangu wiki iliyopita baada ya Arsenal kukubali kumsajili Gyokeres kwa ada ya Pauni 63 milioni. Kati ya hizo, Pauni 55 milioni (Sh192 bilioni) zitalipwa moja kwa moja kwa Sporting na Pauni 8.7 milioni (Sh30 bilioni) zitalipwa kulingana na maendeleo na mafanikio ya mchezaji huyo ndani ya Arsenal.
Hata hivyo fedha hizo za malipo ya ziada ndizo zilichelewesha uhamisho huo kutokana na timu hizo mbili kutofautiana katika mahitaji ya namna fedha hizo zitakavyolipwa.
Lakini juzi Sporting na Arsenal zilikubaliana rasmi na mshambuliaji huyo anatarajiwa kusafiri kwenda Singapore kuungana na kikosi cha timu hiyo ambacho kipo huko kwa kambi ya maandalizi ya msimu mpya.
Gyokeres amekuwa kipaumbele cha Arsenal katika dirisha hili la usajili la majira ya kiangazi akiaminika kwamba ataiimarisha safu ya ushambuliaji ya timu hiyo kutokana na uwezo wake wa kufumania nyavu. Katika msimu wa 2024/2025, Gyokeres ameifungia Sporting Lisbon mabao 54 katika mechi 52.
Kiujumla katika mechi 102 ambazo Gyokeres ameichezea Sporting kwa misimu miwili, Mshambuliaji huyo amepachika mabao 97.
Wakati ikikamilisha mchakato wa uhamisho wa Gyokeres, Arsenal inaripotiwa imeanza harakati za kumnasa Eberechi Eze wa Crystal Palace.
Inaripotiwa kwamba Arsenal ipo tayari kulipa kitita cha Pauni 67.5 milioni (Sh236 bilioni) ambacho Palace wanakihitaji ili kumuachia Eze lakini malipo hayo yawe ya awamu tofauti za muda mrefu.