Karibu usafiri wa treni Dar, lakini tuwe makini nao

Muktasari:
Tangu Dk Mwakyembe atoe kauli hiyo tumeshuhudia marekebisho na ukarabati wa miundombinu umekuwa ukifanyika katika njia hizo za reli.
KUANZIA kesho usafiri wa treni ya abiria kwa wakazi wa Dar es Salaam na vitongoji vyake utaanza rasmi kesho kama ilivyoahidiwa na Serikali.
Hatua hiyo imefikiwa baada ya Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, katikati ya mwaka huu kuahidi kuanzisha usafiri huo kati ya Stesheni na Ubungo Maziwa kwa uapande reli Kati inayotumiwa na kampuni ya Reli Tanzania (TRL) na kati ya Kurasini na Pugu Mwakanga kwa ile ya Shirika la Reli la Tanzania na Zambia (Tazara).
Tangu Dk Mwakyembe atoe kauli hiyo tumeshuhudia marekebisho na ukarabati wa miundombinu umekuwa ukifanyika katika njia hizo za reli.
Ziara iliyofanywa na Kamati ya Bunge pamoja na uongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam chini ya RC Said Meck Sadiq katika njia hizo ikiwamo ya umeonyesha kuwa, matayatisho yamekamilika.
Tunawapongeza wote ambao kwa njia moja, au nyingine wameshiriki kufanikisha mpango huo unafanikiwa kama ilivyopangwa.
Hadi mwisho wa wiki hii mpango huo ulikuwa umefikia hatua ya wadau wa sekta hiyo kujadili kiwango cha nauli ikipendekezwa kuwa iwe Sh800 kwa abiria wa njia ya reli ya kati na 700 kwa ile ya Tazara na Sh100 kwa wanafunzi.
Tunaamini kuwa suala la kiwango cha nauli, ubora wa huduma ambazo zitatolewa katika treni hizi kwa abiria, pia nalo halina budi kuangaliwa kwa umakini mkubwa ili kutowaumiza watumiaji wake.
Tunashauri kwamba wote waliotakiwa kuondosha nyumba, au vibanda vyao vya biashara kando ya njia hizo za reli wafanye hivyo haraka ili kuepusha kutokea ajali na madhara mengine kwao na watumiaji wengine wa huduma hiyo.
Tunasema hatua iliyofikiwa kuelekea kuanza kwa safari hizo itaendelezwa ili hatimaye usafiri huo uanze na hivyo kusaidia kuondoa kero na tatizo sugu la msongamano wa magari na abiria jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo, tunatoa angalizo kuhusu usimamizi na uendeshaji bora na mzuri wa usafiri huo ambao utafanywa na TRL na Tazara ambao nui wazoefu.
Kwa maana hiyo, tunadhani kuwa miradi hii itakuwa endelevu ikiachwa ijiendeshe bila kuingiliwa na wakubwa au watu wenye ushawishi katika jamii, au kugeuzwa kitegauchumi cha wachache watakaonufaika na mapato yatakayotokana na utoaji wa huduma hiyo.
Angalizo jingine tunalitoa kwa watu wenye uwezo kifedha na ambao wamekuwa wakiingia katikati ya Jiji kwa magari yao binafsi, wasifanye hiyo badala yake watume usafiri wa treni hizo ili kupunguza foleni.
Hata hivyo, tunashauri mamlaka zilizopo ziangalie suala la maegesho ya magari na ulinzi katika eneo la Ubungo ili kuwawezesha watu wengi kukubali kuacha magari yao na kupanda treni.
Hili, tunaamini likifanyika, msongamano sugu wa magari katika barabara zetu utakuwa umepata dawa ya kudumu.