Chadema yaja kivingine uchaguzi 2025

Ziara za viongozi
Katika kusisitiza hilo, Mnyika alisema baadhi ya viongozi wa Chadema kama vile Kigaila na John Mrema, mkurugenzi wa itikadi, mawasiliano na mambo ya nje, hawaonekani kwa kuwa wanazunguka mikoani kuwatembelea wanachama.
Alisema Chadema ina watu ambao wamejitolea maisha yao kukitetea chama, akitolea mfano viongozi hao waliokubali kuacha familia zao kwa muda mrefu kwenda kukijenga chama hadi ngazi ya chini.
“Mkitaka kujua kama tumefanya kazi kubwa huko Victoria, angalia jinsi CCM wanavyohangaika kurudi Kanda ya Ziwa; Mwanza, Geita na kwingineko, wanajaribu kupeleka nguvu kuzima moto, lakini moto ule hauzimiki kwa sababu unawaka chini kwa chini,” alisema.
Alisema wamefanikiwa kukiweka chama kwenye roho za watu kama chama mbadala, kama chama kilicho tayari kuleta mabadiliko kwenye maisha ya watu na kitakachorudisha matumaini yao yaliyopotea.
Maridhiano na CCM
Katika hatua nyingine, Mnyika alisema mazungumzo kati ya CCM na Chadema yamekwama kwa sababu chama tawala kimekataa hoja mbili muhimu za Chadema, ambazo ni kupeleka bungeni muswada wa sheria wa kuendeleza mchakato wa Katiba mpya na muswada wa mabadiliko ya Katiba ili kuwezesha matokeo ya kura za urais kuhojiwa mahakamani.
Baada ya kukwama hapo, Mnyika alisema waliwaambia wenzao wa CCM kwamba wakifanya hili na hili, wako tayari mazungumzo hayo yaendelee wakati wowote. Hata hivyo, alisema tangu wakati huo, CCM haijawatafuta tena.
“Toka wakati huo, wao hawajatutafuta tena kutoa mrejesho kama tunaendelea na mazungumzo au hatuendelei na mazungumzo,” alisema.
Alisema CCM wakitaka kurudi waendelee na mazungumzo, Chadema milango yao iko wazi lakini lazima watekeleze yale ambayo Chadema inadhani ni muhimu kwa ajili ya mustakabali mwema wa demokrasia nchini.
Akizungumzia miswada iliyopelekwa bungeni kubadili sheria za uchaguzi na Tume ya Uchaguzi, Mnyika alisema haitoi suluhisho kwa changamoto za kiuchaguzi.
Kwa mfano, alisema muswada wa Sheria ya Tume ya Uchaguzi bado unapendekeza wakurugenzi waendelee kusimamia uchaguzi na Rais bado ana nguvu ya kuteua mwenyekiti wa tume hiyo.
Kutokana na hilo, Mnyika alitoa wito: “Umma ujadili hili jambo na Serikali ipate shinikizo la umma kuhusu miswada ya sheria za uchaguzi kwa njia mbalimbali ili kabla kamati ya Bunge haijaanza, Serikali isikie sauti za wananchi.”
Ujumbe kwa Rais
Alipoulizwa iwapo akipata nafasi ya kukutana na Rais Samia Suluhu Hassan atamwambia nini, Mnyika alisema “aisimamie falsafa yake ya 4R kikamilifu kwa kuwa watendaji wake hawafanyi kama vile malengo yake yalivyo kwenye falsafa hiyo.
“Kwa sasa zile 4R, R ya reform (mabadiliko) imevurugwa, wamepeleka miswada mibovu, aiondoe na atoe mwelekeo sahihi wa reform kwenye nchi. Suala la reconciliation (maridhiano), wamemvuruga, mazungumzo kati ya CCM na Chadema yamekwamishwa, kwa hiyo ajenda yake imekwama, aisimamie.
“Na kama hakuna reform na reconciliation, maana yake kutakuwa hakuna rebuilding (kujenga upya). Arudishe nchi katika mkondo sahihi wa zile 4R alizokuwa anazisema, yeye ndiye anaweza kulifanya hilo,” alisema Mnyika.