TACAS yaunga mkono pendekezo la ada kuboresha huduma, usafirishaji mizigo
Muktasari:
- lengo kubwa ni kuhakikisha bandari za Tanzania zinakuwa za kisasa, zenye uwezo mkubwa wa kuhudumia mizigo mingi kwa haraka na ufanisi zaidi.
Dar es Salaam. Chama cha Mawakala wa Forodha Tanzania (TACAS) kimesema pendekezo la ada ya asilimia 4.5 ya uendelezaji wa Miundombinu mipya ya Bandari (PID) inalenga kusaidia maboresho makubwa ya bandari nchini ili kuongeza ufanisi wa huduma za usafirishaji wa mizigo.
Akizungumza mkoani Mtwara, Juni 2, 2026 katika Mkutano wa Wadau wa Watumiaji wa Bandari ya Mtwara kuhusu ada hii ya kuendeleza Miundombinu mipya ya Bandari, Mwenyekiti wa TACAS, Ephraim Mwankusye, amesema fedha zitakazopatikana zitaelekezwa katika utekelezaji wa miradi mbalimbali mipya ya kuendeleza miundombinu ya Bandari za Mtwara, Dar es Salaam, Tanga na maendeleo ya Bandari ya Bagamoyo pamoja na ujenzi wa miundombinu ya mafuta katika bandari mbalimbali nchini.
Amesema lengo kubwa ni kuhakikisha bandari za Tanzania zinakuwa za kisasa, zenye uwezo mkubwa wa kuhudumia mizigo mingi kwa haraka na ufanisi zaidi.
Tozo hiyo ya PID ni fedha inayokusanywa kutoka kwa watumiaji wa bandari kwa ajili ya kugharamia maendeleo na maboresho ya miundombinu ya bandari nchini.
Kwa mujibu wa pendekezo hilo, asilimia 4.5 ya tozo itaelekezwa katika miradi ya kuboresha bandari, magati, reli, matenki ya mafuta pamoja na barabara zinazosaidia usafirishaji wa mizigo.
Nao Wadau mbalimbali walioshiriki Mkutano huo, wameunga mkono Ada hiyo ya uendelezaji wa miundombinu mipya ya Bandari (PID) wakisema italeta mageuzi makubwa katika kuhudumia shehena katika bandari zetu.