Meya wa Iringa ataka watoto walindwe
Muktasari:
- Meya wa Manispaa ya Iringa, Ibrahimu Ngwada, ameitaka jamii kuwalinda watoto na kutofumbia macho ukatili dhidi yao kwa kuwa vitendo hivyo vinaathiri ukuaji wao kiakili.
Iringa. Meya wa Manispaa ya Iringa, Ibrahimu Ngwada ameitaka jamii kuwalinda watoto na kutofumbia macho ukatili dhidi yao kwa kuwa vitendo hivyo vinaathiri ukuaji wao kiakili.
Amesema mtoto aliyefanyiwa ukatili wa kijinsia, hawezi kuwa na maendeleo mazuri kwenye makuzi yake kwa sababu muda mwingi atakuwa na hofu hasa anapokumbuka alichofanyiwa.
Akizungumza na Mwananchi, Ngwada amesema kumekuwa na kesi nyingi za ukatili dhidi ya wanawake na watoto jambo linalopaswa kukemewa na kila mwanajamii.
“Inasikitisha sana kuona vitendo vya ukatili kwa watoto na wanawake vinafanywa na watu wenye akili timamu kabisa tena watu wa karibu. Kwanini jamii inakaa kimya jamani? Suala hili linatakiwa kukemewa kwa nguvu zote,” amesema Ngwada.
Amesema inawezekana kukomesha matukio hayo ikiwa jamii itashirikiana na mamlaka husika katika kuwafichua waharifu na sio kuwaficha kama baadhi ya familia zinavyofanya.
Kwa upande wake Afisa Ustawi wa Jamii Manispaa ya Iringa, Tiniel Mbaga amesema kihalisia msingi wa vitendo hivyo ni familia, wazazi na walezi.
"Ukatili huu unafanyika kwa kificho hivyo ulinzi kwa wanawake na watoto unakuwa mdogo kwa sababu hawajitokezi kuleta malalamiko hayo," amesema Mbaga.
Mbaga amesema kuwa ukatili unasababishwa na mambo kama ulevi, mila na desturi, mfumo dume na kutokuwepo kwa hali za kuheshimu watoto majumbani.