Maandamano ya Gen Z, Ruto asisitiza mikono yake safi

Rais wa Kenya, William Ruto wakati akihutubia Taifa mubashara kuhusu maandamano nchini humo Juni 25, 2024.

Rais wa Kenya, William Ruto amesisitiza mikono yake haijachafuka damu kutokana na mauaji yaliyotokea nchini humo, baada ya waandamanaji kukabiliana na polisi.

Mamia ya Wakenya waliandamana Jumapili jijini Nairobi, kuwaenzi wale waliofariki katika maandamano ya kuipinga Serikali wiki iliyopita. Inadaiwa watu 30 waliuawa katika maandamano hayo.

Rais Ruto, aliyekuwa akizungumza katika mahojiano na waandishi wa habari Ikulu, amesema maofisa wa polisi walitekeleza majukumu yao kwa njia huru wakati wa maandamano hayo.

Tume ya Haki za Kibinadamu ya Kenya (KHRC) imesema watu 23 walifariki dunia kwa kupigwa risasi na polisi nchini humo. Mbali na hayo, kulikuwa na zaidi ya watu 50 waliokamatwa, 22 kutekwa nyara na zaidi ya 300 kujeruhiwa. Rais Ruto hata hivyo alishikilia kuwa ni watu 19 ndio waliofariki.

Kufuatia ghasia hizo, Ruto ametangaza kubadili msimamo mapema wiki iliyopita, akisema “atawasikiliza wananchi” na hatasaini mswaada wa fedha kuwa sheria.

Akizungumzia vifo hivyo, Rais Ruto amesema:“Hii ni hali ya kusikitisha sana. Kama Taifa la kidemokrasia, hali kama hiyo haikutakiwa kutawala mjadala wetu...uchunguzi utafanyika kuhusu namna watu hao 19 walivyofariki."

Amesema:"Polisi walijaribu kufanya wawezavyo, iwapo walitumia nguvu kupita kiasi, tuna njia za kuhakikisha kwamba hali hiyo inashughulikiwa.”


'Tutawakamata' wahalifu

Rais Ruto ameonya wale walioshambulia Bunge pia watawajibishwa.

“Wahalifu walijipenyeza na kusababisha ghasia,” amesema:"Walioshambulia Bunge na mahakama wapo wameonekana kwenye CCTV (kamera za usalama)."

“Wengi wao wako mbioni wamekimbia, lakini tutawakamata,” ameongeza.

Akirejea uamuzi wake wa kufuta Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2024, Ruto alisema: "Ina maana kwamba tumerudi nyuma karibu miaka miwili" na kumaanisha kuwa Serikali italazimika kukopa sana.

Lakini amekiri: "Tulipaswa kuwasiliana vizuri zaidi, nikipewa nafasi ya kueleza watu wa Kenya muswada wa fedha ulikuwa unahusu nini na ungewafanyia nini, basi kila Mkenya angekubaliana nami."

Ghasia hizo hazijawahi kutokea katika historia ya nchi hiyo tangu ilipopata uhuru wake kutoka kwa Uingereza mwaka 1963.

Jumamosi iliyopita, mamia ya watu walikusanyika katika bustani ya Uhuru Park katikati mwa Nairobi kutokana na rufaa kwenye vyombo vya habari.

Baada ya kuimba na kuwasha mishumaa, walipeperusha bendera za Kenya na kuimba, huku wakipita hospitalini ambako baadhi ya waandamanaji waliojeruhiwa wanapatiwa matibabu. Waandamanaji walitawanyika kwa amani alasiri.

Maandamano yalianza baada ya Serikali ya Rais Ruto kutangaza sera mpya za uchumi ambazo ziliongeza kodi na kupunguza ruzuku kwenye bidhaa muhimu.

Hatua hizo zilikusudiwa kupunguza nakisi ya bajeti na kulipa madeni ya taifa. Hata hivyo, vijana wa Gen Z, ambao tayari wanakabiliwa na ukosefu wa ajira na gharama kubwa za maisha, waliona kuwa sera hizoi ni mzigo kwao.

"Hatua hizi za Serikali zimeongeza gharama za maisha na kuzidisha hali ya ukosefu wa ajira kwa vijana," amesema John Kamau, mwanaharakati wa haki za kijamii. "Hatuwezi kukaa kimya wakati maisha yetu yanazidi kuwa magumu."

Kizazi cha Gen Z kimeonyesha uwezo mkubwa wa kujipanga na kuandaa maandamano kupitia mitandao ya kijamii kama Twitter, Facebook na Instagram. Kupitia majukwaa hayo, vijana wamehamasishana, kushirikiana mawazo na kupanga mikakati ya maandamano.

"Mitandao ya kijamii imekuwa nyenzo muhimu kwetu," amesema Mary Wanjiku, mmoja wa waandaaji wa maandamano. "Imetusaidia kuunganisha nguvu na kufanya sauti zetu zisikike."

Ingawa Serikali ya Ruto imejaribu kutuliza maandamano kwa kutoa ahadi za kufanya marekebisho kadhaa katika sera zake, ikiwa ni pamoja na kukataa kusaini muswada wa fedha, hatua hizo hazijawaridhisha vijana wengi ambao wanataka mabadiliko ya haraka na makubwa zaidi.

Kilichokuwa kwenye muswada wa fedha, bajeti ya Sh4 trilioni nne (dola bilioni 31.1) ilikuwa kubwa zaidi katika historia ya Kenya na ilijumuisha ongezeko la ushuru kwa bidhaa za msingi kama vile mkate na mafuta.

Waandamanaji walisema hatua hizo zitawagusa maskini na wafanyakazi, ambao tayari wanapambana na mzozo mkubwa wa gharama ya maisha.

Lakini Ruto na Serikali yake walitetea hatua hiyo, ambayo ingeongeza takriban dola bilioni 2.7 kama ushuru wa ziada, ikihitajika kupunguza deni la Kenya ambalo linafikia takriban Sh10 trilioni, karibu asilimia 70 ya Pato la Taifa.

Takwimu za Hazina za Aprili zilionyesha kuwa Serikali ilitumia takriban Sh1.2 trilioni kulipia deni kati ya Julai 2023 na Machi 2024, ikilinganishwa na Sh1.1 trilioni za mishahara na miradi ya maendeleo kama vile barabara, huduma za afya, elimu na miundombinu mingine muhimu.

Kulingana na takwimu za Biashara na Maendeleo za Umoja wa Mataifa za mwaka wa 2021, Kenya inatumia asilimia 4.4 ya Pato la Taifa katika elimu na asilimia 1.9 tu kwa afya.


Kizazi cha Gen Z na mabadiliko Kenya

Kizazi cha Gen Z, ambacho kinaundwa na vijana waliozaliwa kati ya mwaka 1997 na 2012, kimeibuka kama nguvu ya kushinikiza mabadiliko nchini Kenya.

Gen Z wamekuwa wakijitokeza kwa wingi kupitia mitandao ya kijamii na intaneti. Simu zao za mkononi na mitandao vimekuwa vyombo vyao vya kuungana, kutoa sauti na kueleza hasira zao dhidi ya sera za kiuchumi na utawala.

Kupitia majukwaa kama Twitter Space na TikTok, vijana wamejadili masuala kama ukali wa maisha, gharama kubwa ya bidhaa, ubadhirifu wa fedha za umma na ukosefu wa ajira.

Maandamano yao yalianza jijini Nairobi na kuenea hadi maeneo mengine ya Kenya kama Mombasa, Kisii, Kisumu, Nakuru, Nyeri na Nanyuki.

Vijana walijitokeza barabarani wakiwa na mabango, wakipinga mapendekezo ya kodi yaliyokuwa hayawapendezi. Walitumia weledi wao katika mitandao ya kijamii kuungana na kutoa sauti zao.

Vijana hawa walifanikiwa kushinikiza Serikali kubadilisha baadhi ya mapendekezo ya kodi. Rais Ruto alisalimu amri na kuondoa muswada wa fedha uliopitishwa na Bunge.

Walionyesha uwezo wao wa kuathiri siasa na kuonyesha umuhimu wa sauti zao katika kuleta mabadiliko.

Kwa kifupi, Gen Z wameonyesha ujasiri na uwezo wa kushinikiza mabadiliko kupitia mitandao ya kijamii na maandamano. Sauti zao zimeleta mabadiliko muhimu katika sera za nchi.


Gen Z na mustakabali wa siasa za Kenya

Kizazi cha Gen Z kina nafasi kubwa ya kuleta mabadiliko katika siasa za Kenya. Ushiriki wao katika michakato ya kisiasa kupitia mitandao ya kijamii na maandamano umeonyesha kuwa wanaweza kuwa na ushawishi mkubwa katika kuunda sera na uamuzi wa kisiasa. Hii inatoa matumaini kwamba kizazi hiki kitaendelea kushinikiza mabadiliko katika siasa za nchi.

Pamoja na changamoto zinazowakabili vijana wa Gen Z, kuna fursa nyingi zinazoweza kuwasaidia kuleta mabadiliko katika siasa za Kenya.

Kupitia teknolojia na mitandao ya kijamii, wanaweza kuendelea kuhamasisha na kuelimisha jamii kuhusu masuala mbalimbali ya kisiasa. Pia, kwa kujiunga na vyama vya siasa na kugombea nafasi za uongozi, wanaweza kuleta mabadiliko kutoka ndani.