Mastaa na kundi la uchumba, ndoa zisizodumu

Muktasari:

  • Maana hiyo imekuwa tofauti kwa mahusiano na ndoa za baadhi ya watu maarufu Bongo. Kwa miaka ya hivi karibuni watu wameshuhudia uhusiano na ndoa nyingi ambazo zilitikisa kupitia mitandao ya kijamii, lakini mwisho wake huangukia pua.

Ndoa, ni muungano ulioidhinishwa kisheria na kijamii, kwa kawaida kati ya mwanamume na mwanamke hukubaliana kwa pamoja kuingia katika hatua hiyo pindi wamalizapo kujuana kwa kina katika uchumba.

Maana hiyo imekuwa tofauti kwa mahusiano na ndoa za baadhi ya watu maarufu Bongo. Kwa miaka ya hivi karibuni watu wameshuhudia uhusiano na ndoa nyingi ambazo zilitikisa kupitia mitandao ya kijamii, lakini mwisho wake huangukia pua.

Huku sababu kubwa zikitajwa ni tamaa, kupishana umri, kufunga ndoa kwa lengo la kutafuta kiki, kutokuwa na uvumilivu. Na haya ndiyo uhusiano na ndoa za baadhi ya mastaa ambazo hazijadumu.


Diamond, Zari, Tanasha, Hamisa

Kati ya mahusiano ambayo yalipamba moto kupitia mitandao ya kijamii ni hili la mwanamuziki Naseeb Abdul, maarufu kama Diamond na aliyekuwa mwanamuziki na mfanyabiashara Zarinah Hassan ajulikanaye kama ‘Zari The Boss Lady’,  ambayo yaliripotiwa kuanza mwishoni mwa mwaka 2014 na kuvunjika 2018, huku wakiwa wamebahatika kupata watoto wawili ambao ni Tiffah na Nillan.


                       

Zari aliripoti kuachana na Diamond kupitia mitandao ya kijamii siku moja kabla ya Valentine Day mwaka 2018, kwa kuposti ua jeusi lililoambatana na ujumbe wa kuachana.
Lakini kufuatia  mienendo yake iligundulika wakati yupo kwenye mahusiano na Zari pia alikuwa penzini na mwanamitindo Hamisa Mobetto, wakaachana 2020.

Hata hivyo, Diamond baada ya kuachana na Hamisa Mobetto aliamua kuibukia nchini Kenya ambapo alikuwa na uhusiano na mwanamuziki Tanasha Donna, pia alibahatika kupata naye mtoto mmoja aitwaye Naseeb Junior, wawili hao waliachana mwanzoni mwa mwaka 2022, ambapo Diamond kwa sasa anahusishwa kutoka kimapenzi na msanii wake, Zuhura Othman, maarufu kama Zuchu.


                      

Mbali na hayo, Diamond aliwahi kutoka kimapenzi na Miss Tanzania 2006 Wema Sepetu na kuachana kutokana na usaliti uliokuwa ukiendelea baina yao, kama alivyowahi kueleza Wema kwenye moja ya mahojiano yake.
 
Harmonize, Wolper, Sarah na Kajala

Yakizungumziwa mahusiano yaliyowahi kutikisa Bongo na baadaye kusambaratika kama upepo ni ya mkali Rajab Kahali, maarufu kama Harmonize na muigizaji Jackline Wolper, hili lilikuwa penzi la kwanza kwa Konde Boy kufikishwa kwenye mitandao ya kijamii wakati ameanza kujipata akiwa kwenye lebo ya ‘WCB’.


                       

Kwa mara ya kwanza wawili hao walionekana wakiwa kwenye penzi zito katika birthday party ya mtoto wa Mosse Iyobo na Aunty Ezekiel mwaka 2016.

Penzi la wawili hao lilifika tamati mwaka 2017, ambapo kutokana na tetesi kwenye mitandao ya kijamii, ilielezwa kuwa Harmonize alipewa muigizaji huyo ili amtoa ushamba.

                       

Baada ya Harmonize kuachia ngazi kwa Wolper alizama kwa raia wa Italia, Sarah Michelotti, penzi  lao lilikolea nazi mpaka kupelekea wawili hao kufunga ndoa ya siri ambayo ilivunjika mwaka 2020, baada ya Sarah kugundua kuwa Harmonize alikuwa na mtoto nje ya ndoa.

Konde Boy, hakuishia hapo, aliingia kwenye penzi zito na muigizaji mkongwe nchini, Kajala Masanja, penzi lililokuwa na ‘drama’ za kutosha kupitia mitandao ya kijamii, za kuachana, kurudiana, kuvishana pete kupeana magari lakini nalo halikufika mbali, wakapigana chini, huku sababu zikiwa ni zile zile usaliti.


Manara, Naheeda, Rushaynah, Rubynah

Ukiachilia mbali  uhusiano wa mastaa wa muziki, kuna yale ambayo yametikisa mitandao ya kijamii ya aliyekuwa Msemaji wa Klabu ya Yanga, Haji Manara, licha ya Haji kufunguka kupitia mitandao ya kijamii akidai kuwa baadhi ya wanawake aliowaoa hawakutulia, walifuata umaarufu wake.

                      

Manara alianza kwa kufunga ndoa na mdogo wa DC wa Pangani, Zainab Abdallah, Naheeda Abdallah mwishoni mwa mwaka 2020, ambapo ndoa ya wawili hao ilichukua miezi kadhaa ya kuwa pamoja na kuoa mke wa pili ambaye alikuwa ni mfanyabiashara Rubynah na walibahatika kupata mtoto mmoja wa kiume aitwaye Ghalib Haji Manara.

                    

Mwaka 2022, Manara alivuta jiko jingine ikiwa tayari wakati huo ameshaachana na Naheeda, ambapo alimuoa Rushaynah, ndoa ambayo ilizua mengi mpaka kupelekea kuachana kwa kutoleana maneno kwenye mitandao ya kijamii.

Katika mahojiano na mama mzazi wa Haji Manara katika ndoa  ya Manara na Rushaynah, alieleza kuwa mpaka kufikia hapo Manara amewahi kuoa wanawake wanne ambapo Rushaynah akiwa mke wa tano.

                       

Hata hivyo, Manara kwa sasa yuko katika penzi zito ambalo alifunga ndoa na muigizaji, aliyekuwa mke wa Dulla Makabila, Zaiylissa.

Rayvanny, Paula Kajala
Mwaka 2020, mtoto wa Kajala Masanja, Paula Kajala na Rayvanny waliibukia penzini, hata hivyo, wawili hao walifanikiwa kudumu kwa kipindi cha mwaka mmoja tu ambapo mwaka 2022 waliachana rasmi kwa kurushiana maneno kupitia mitandao ya kijamii.


Esma Khan na Yahya Msizwa

Moja kati ya ndoa ambayo ilichukua kipindi kifupi sana na ambayo ilitrendi kupitia mitandao ya kijamii ni ya mdogo wa mwanamuziki Diamond, Esma Platnumz na mfanyabiashara Yahya Msizwa ambayo Julai, 2020, alifungwa ambapo Esma alikuwa mke wa tatu.


                         

Licha ya harusi yao kuwa ya kifahari, ndoa hiyo ilifanikiwa kudumu kwa miezi mitano tu kisha ikavunjika.

Mbali na hiyo Esma aliwahi kufunga ndoa na Petit Man Wakuache 2015 na walibahatika kupata mtoto wa kike aitwaye Taraji.

                     

Hata hivyo kwa sasa amefunga ndoa na Meneja Jembe One Alhamisi iliyopita Februari 22 mwaka huu, baada ya ndoa hiyo alifunguka kuwa hiyo aliyoifunga ilikuwa ni ya tano