Saudi Arabia yapewa Kombe la Dunia 2034

Hatimaye Shirikisho la soka la Kimataifa (Fifa), limetangaza Fainali za Kombe la Dunia 2034 zitafanyika Saudi Arabia, huku nchi za Hispania, Ureno, na Morocco zikiwa wenyeji wa pamoja wa mashindano ya 2030.
Pia imeelezwa mechi tatu za Kombe la Dunia la 2030 zitachezwa Amerika Kusini katika mataifa ya Argentina, Paraguay, na Uruguay, ili kuadhimisha miaka 100 tangu kuanzishwa kwa mashindano hayo.
Uthibitisho wa wenyeji wa mashindano yote mawili ulifanyika katika kikao maalum cha Mkutano wa Fifa kilichofanyika Jumatano kupitia kura.
Wajumbe wote 211 wa Fifa kutoka mataifa wanachama walihudhuria kikao hicho kwa njia ya mtandao.
Kulikuwa na upigwaji wa kura mara mbili tofauti zilzopigwa kuthibitisha wenyeji wa mashindano hayo.
Kura ya kwanza ilichagua Uruguay, Paraguay, na Argentina kuwa wenyeji wa maadhimisho ya miaka 100.
Kura ya pili ilithibitisha wenyeji watatu wa mashindano ya 2030 pamoja na Saudi Arabia kama mwenyeji wa mashindano ya mwaka wa 2034.
Hii ni hatua muhimu katika historia ya soka, huku shirikisho la Fifa likionyesha nia ya kuleta mshikamano wa kimataifa kupitia fainali hizo kubwa zaidi duniani.
Kuchaguliwa kwa Morocco kati ya mataifa matatu wenyeji wa 2030 kunamaana kuwa kombe hilo litachezwa kwa mara ya pili Afrika, mara ya kwanza ilikuwa 2010, Afrika Kusini.
Kijiografia Morocco ipo karibu na mataifa hayo ya Ulaya hivyo kutakuwa na wepesi wa muingiliano wakati wa fainali hizo.