Aucho kujiunga Singida Black Stars
Muktasari:
- Mwanaspoti lilisharipoti uwepo wa mazungumzo ya Singida Black Stars kumnasa kiungo huyo raia wa Uganda na sasa ni rasmi amemwaga wino huku muda wowote kuanzia sasa atatambulishwa rasmi tayari kwa maandalizi ya msimu wa 2025/26.
Singida Black Stars imekamilisha usajili wa aliyekuwa kiungo wa Yanga, Khalid Aucho ikimpa mkataba wa miaka miwili.
Tayari mazungumzo ya Singida Black Stars kumnasa kiungo huyo raia wa Uganda yameenda vizuri na sasa ni rasmi amemwaga wino huku muda wowote kuanzia sasa atatambulishwa rasmi tayari kwa maandalizi ya msimu wa 2025/26.
Chanzo cha kuaminika kutoka Singida Black Stars, kililiambia Mwananchi tayari wamemnasa kiungo huyo kwa mkataba wa miaka miwili na atakuwa sehemu ya malengo yao msimu huu ndani na kimataifa.
“Tulipokuwa tunauza wachezaji tulikuwa na mipango mingine mikubwa ambayo siku ya Singida Big Day ndiyo tutatoa majibu kuwa bado tutakuwa na timu bora na ya ushindani, sio Aucho tu, kuna nyota wengine bora,” kilisema chanzo hicho na kuongeza.
“Tuna malengo makubwa, kinachozingatiwa sasa ni uzoefu na ubora, kila mmoja anafahamu ubora wa Aucho akifanya mambo makubwa kwenye ligi yetu, tunaamini atafanya hivyo pia akiwa Singida Black Stars.”
Alisema wamefanya uamuzi wa kumnasa kiungo huyo kutokana na uzoefu na ubora alionao huku wakiamini atakuwa mchezaji kiongozi katika timu yao kutokana na kuwa na uzoefu wa ndani na kimataifa.
Aucho anaifahamu vizuri Ligi ya Bara kutokana na kuichezea Yanga misimu minne tangu alipojiunga nayo Agosti 2021, akitokea Misr Lel Makkasa SC ya Misri na kuondoka mwisho wa msimu wa 2024-2025 na muda wote huo amekuwa kiungo namba moja na mchezaji wa kutumainiwa eneo la ukabaji.
TIMU ALIZOPITA
2009–2010 Jinja Municipal
2010–2012 Water
2012–2013 Simba
2013–2014 Tusker
2015–2016 Gor Mahia
2016 Baroka
2017 Red Star Belgrade
2017 OFK Beograd
2017–2018 East Bengal
2018–2019 Churchill Brothers
2019–2021 Makkasa
2021– Yanga