Utafiti: Ujuzi laini kikwazo cha wahitimu kwenye ajira
Muktasari:
- Matokeo ya utafiti huo yanabainisha kuwa mbinu za mafunzo pekee hazitoshi kupelekea ajira isipokuwa ziwe zimejengwa kwa makusudi kukuza ujuzi huo.
Dar es Salaam. Mfumo wa elimu nchini Tanzania unakabiliwa na changamoto ya kimyakimya lakini yenye gharama kubwa, ambapo wahitimu wanaondoka vyuoni bila kuwa na ujuzi laini maarufu Kiingereza kama ‘soft skills’ unaozidi kuhitajika kwa waajiri.
Utafiti wa hivi karibuni uliotolewa katika jarida la Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) la ‘Journal of Educational Management and Policy Issues’ unaonesha kuwepo kwa pengo la kimuundo katika namna taasisi za elimu ya juu zinavyowaandaa wanafunzi kwa mazingira halisi ya kazi za kisasa.
Utafiti wa mwaka 2025 uliofanywa na Noel Mkwizu, Albino Tenge na Lily Makalanga unaonyesha kuwa ujuzi kama mawasiliano, kufanya kazi kwa pamoja, uwezo wa kuhimili mabadiliko na kutatua matatizo si nyongeza tu, bali ni mhimili mkuu wa ajira.
Matokeo ya utafiti huo yanabainisha kuwa mbinu za mafunzo pekee hazitoshi kuchangia ajira isipokuwa ziwe zimejengwa kwa makusudi kukuza ujuzi huo.
Utafiti unaonyesha pia kuwepo kwa uhusiano mkubwa kati ya ujuzi huo na ajira, jambo linalomaanisha kuwa wahitimu wenye uwezo mzuri wa kijamii na kubadilika kulingana na mazingira, wana nafasi kubwa zaidi ya kupata ajira.
Nchini Tanzania, waajiri kwa muda mrefu wamekuwa wakilalamikia ukosefu wa utayari wa wahitimu kuingia katika soko la ajira. Utafiti huo unathibitisha hali hiyo, ukieleza kuwepo kwa pengo kubwa kati ya ujuzi walionao wahitimu na ule unaohitajika sokoni” hasa katika eneo la ujuzi laini.
Mchambuzi wa masuala ya elimu, Dk Hemed Mvula, katika mazungumzo na Mwananchi, Aprili 15, 2026, alisema mabadiliko ya matarajio ya waajiri hayaepukiki.
“Mahali pa kazi leo ni pa mabadiliko ya haraka. Waajiri wanahitaji watu wanaoweza kufikiri, kuwasiliana na kubadilika. Maarifa ya darasani pekee hayatoshi tena,” alisema.
Kimataifa, mwelekeo huu unaendelea kushika kasi. Shirika la Organisation for Economic Co-operation and Development (OECD) linaeleza kuwa waajiri wengi sasa wanatumia mbinu ya “ujuzi kwanza” (skills-first), wakitoa kipaumbele kwa kile mtu anachoweza kufanya kuliko alichosomea.
Ujuzi unaoelezwa mara nyingi kama upande wa kibinadamu wa kazi, unaathiri namna mtu anavyowasiliana, kutatua matatizo na kukabiliana na mabadiliko.
Utafiti wa UDOM unaonyesha kuwa hata programu bora za mafunzo hushindwa kuboresha ajira iwapo hazijajumuisha kwa makusudi ujuzi huo. Watafiti wanauelezea ujuzi laini kama “daraja” linalounganisha elimu na ajira.
Mtaalamu wa elimu ya juu, Dk Steven Tweve, anasema umahiri wa kiufundi pekee hautoshi tena.
“Unaweza kuwa na mhitimu mwenye uwezo mkubwa kitaaluma, lakini kama hawezi kuwasiliana, kufanya kazi kwa timu au kutatua matatizo, waajiri watasita. Huu ndio ujuzi unaomfanya mtu aajirike,” alifafanua.
Chanzo kikuu cha tatizo hili ni namna elimu inavyotolewa. Kwa miaka mingi, taasisi za elimu ya juu nchini zimejikita zaidi katika nadharia na mitihani, mara nyingi zikisahau ujuzi wa vitendo na wa kijamii.
Ingawa maboresho kama mfumo wa mafunzo unaozingatia umahiri (CBT) yameanzishwa, utafiti unaonyesha kuwa hufanikiwa zaidi pale unapochanganywa na uzoefu wa moja kwa moja kazini, kama vile mafunzo kwa vitendo (internships) na ujifunzaji kazini (apprenticeships).
Programu zinazochanganya darasa na mazingira ya kazi ndizo zinaonesha matokeo bora zaidi, zikithibitisha umuhimu wa mafunzo ya vitendo.
“Ujifunzaji kwa vitendo ni muhimu sana. Wanafunzi wanahitaji kuingia katika mazingira halisi ya kazi ili kukuza ujuzi huu kwa njia ya asili,” alisema Dk Tweve.
Hata hivyo, taasisi nyingi bado zinakosa miundombinu, ushirikiano na sekta binafsi pamoja na rasilimali za kutosha kuwezesha fursa hizo.
Athari za changamoto hii hazibaki kwa wahitimu pekee, bali zinaigusa pia uchumi wa Taifa. Kila mwaka, maelfu ya wahitimu huingia katika soko la ajira, lakini kutokuwiana kati ya elimu na mahitaji ya waajiri kunachangia ukosefu wa ajira na ajira zisizo na tija, hasa kwa vijana.
Kwa mujibu wa Benki ya Dunia (WB), upungufu wa ujuzi unapunguza uzalishaji na kudhoofisha ushindani wa nchi katika uchumi wa dunia, hali inayosababisha kupotea kwa fursa kwa watu binafsi na sekta mbalimbali.
Wataalamu wanaeleza kuwa kutatua changamoto hii kunahitaji mabadiliko ya kimfumo. Vyuo vikuu vinapaswa kubadili mitaala ili kujumuisha ujuzi laini katika ufundishaji na tathmini, ikiwemo kazi za vikundi, mawasilisho, mafunzo kwa vitendo na ujifunzaji unaotatua matatizo halisi.
Aidha, ushirikiano imara kati ya vyuo na sekta ya ajira ni muhimu ili kuhakikisha mafunzo yanaendana na mahitaji ya soko.
Katika ngazi ya sera, uwekezaji katika miundombinu, mafunzo ya walimu na maboresho ya mitaala ni muhimu ili kuimarisha ujifunzaji wa vitendo.
Utafiti wa UDOM unatuma ujumbe wazi: mustakabali wa elimu hauko tu katika maarifa, bali katika uwezo wa kuyatumia.
Wakati Tanzania ikiendelea kujenga uchumi shindani unaotegemea maarifa, kuziba pengo la ujuzi laini kunaweza kuwa moja ya mageuzi muhimu zaidi katika sekta ya elimu.
Kwa sababu katika soko la ajira la leo, si tu kile unachojua kinachohesabika bali ni namna unavyoweza kukitumia.